Sekta binafsi walia na TRA
- Imeandikwa tarehe 15 Juni 2012
- By Sifa Lubasi, Dodoma
- Imesomwa mara: 473
TAASISI ya Sekta binafsi nchini (TPSF) imesema kuwa uwezo mdogo wa kukusanya kodi wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) unasababisha bajeti kuegemea kuongeza kodi kwenye bidhaa za vinywaji ambavyo vinaaminika kuwa ni chanzo cha mapato yao.
Pia taasisi hiyo imeshauri Serikali ianzishe utaratibu wa kuajiri kwa mikataba ya miaka mitatu tu ili kuweza kuwa na nidhamu katika utendaji kazi na matumizi ya fedha za umma pia.
Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa TPSF, Godfyey Simbeye wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa juu ya kauli ya taasisi hiyo baada ya Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa kuwasilisha bajeti ya Serikali jana.
Alisema kuwa hii inaonesha dhahiri kuwa TRA haina orodha kamili ya walipa kodi ambao hali ambayo kwa kiasi kikubwa ndiko kiasi kikubwa cha mapato kinakopotea na hivyo kujikuta wakilazimika kukandamiza kodi kubwa katika vinywaji.
Alisema kuwa, uamuzi huu wa kuongeza bajeti katika vinywaji haujafanyika katika bajeti hii ya 2012/2013 bali inafanyika karibu bajeti zote katika kila mwaka.
“Wenzetu wa nchi ya Kenya, katika bajeti yao ya mwaka jana hawakugusa kabisa kupandisha kodi katika vinywaji, inaonesha wanakusanya kodi yao katika maeneo mengine,” alisema Mkurugenzi huyo.
Aidha aliongeza kuwa, ni jambo la kushangaza pale ambapo Wabunge walishangilia baada ya kusikia Waziri wa Fedha na Uchumi, alipotangaza kuongeza kodi katika sigara na bia kwa asilimia 25 ili kuweza kuwadhibiti walevi.
Alisema kuwa hivi sasa Tanzania ina watu milioni 45, lakini walipa kodi ni watu 500 hali ambayo huchangia Serikali kushindwa kukusanya mapato stahiki na kuendelea kunyonya walipa kodi wadogo.
“Labda vitambulisho vya taifa vitasaidia nchi hii kuweza kukusanya kodi na kuacha kuangalia kwenye bia na soda,” alisema.
Pia alibainisha kuwa, kama sekta binafsi haikupendekezwa na Serikali kutenga asilimia 70 kwenda kwenye matumizi ya kawaida huku asilimia 30 kwenda kwenye shughuli za maendeleo hali ambayo inaonesha kuwa hakutakuwa na ushindani kwenye biashara.
“Sekta binafsi inapendekeza angalau asilimia 65 ingetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na kwenye shughuli za maendeleo iwe asilimia 35 ili kwenda sambamba na soko la pamoja la Afrika Mashariki,” alisema.
Alisema kuwa, bajeti haikueleza kama Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) atawezaje kuzuia matumizi mabaya ya fedha za umma.
Simbeye alisema kuwa, suala la kuvutia uwekezaji linasuasua kutokana na kutokuwa na benki ya ardhi kwani hakuna ardhi inayotengwa kwa ajili ya uwekezaji katika kilimo.
“Serikali ifikirie kuwa na benki ya ardhi na wangeanza na mikoa mitano kama majaribio, suala la ardhi lingetengewa bajeti hilo pia lingerahisisha hata ukusanyaji wa kodi,” alisema.
Pia alitaka leseni isiwe chanzo cha kukusanya mapato kwenye Halmashauri na kuangaliwa kwa mikakati ya kukuza viwanda ambayo bado haijawekwa vizuri.
Aidha alisema kuwa bajeti ya mwaka huu haiwezi kubadilisha maisha ya Mtanzania kwa kiwango kilichotarajiwa kwani haikuongelea suala la bei ya mafuta.


