Watakiwa kuzingatia mafunzo

SERIKALI imewaagiza  wawezeshaji wa kitaifa wanaoshiriki mafunzo  ya kujenga ujuzi  wa kuibua  hadithi za mafanikio za kujifunza za mfano katika kuboresha ujifunzaji na ufundishaji,  kuzingatia mafunzo hayo vyema na kuhakikisha  yanaleta tija katika maeneo mengi nchini.

Agizo hilo limetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia , Dkt. Francis Michael leo tarehe 24/11/2022  mjini Morogoro wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya wawezeshaji wa kitaifa.

Advertisement

Mafunzo hayo yameandaliwa na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) kupitia programu ya Shule Bora  inayofadhiliwa na shirika la UKaid.

Dkt. Michael amesema, serikali imewekeza katika mafunzo ya walimu kazini, hivyo wanapaswa kuzingatia na kupeleka ujuzi waliopata kwa washiriki waliokusudiwa katika ngazi ya mkoa na halmashauri.

“Hakikisheni mnazingatia mafunzo haya na kushiriki kikamilifu ili kuendelea kushirikishana namna hadithi za mafanikio za kujifunza za mfano zinavyoweza kuboresha  ujifunzaji na ufundishaji shuleni” amesema Dkt. Michael.

Pia amemshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kujenga uhusiano mzuri  na  wadau wa maendeleo ya elimu nchini  ambao wanaendelea kuwezesha kuwepo kwa miradi mingi ya elimu nchini.

Kwa upande wake Mshauri Mkuu kiongozi wa programu ya Shule Bora  Vincent Katabalo amesema kuwa  wataendelea kutekeleza mradi wenye lengo la  kuongeza ubora wa elimu nchini.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dkt. Aneth  Komba amesema kuwa mafunzo hayo ni nyenzo muhimu  kuleta ufanisi katika kutekeleza  mitaala ili kuboresha  ufundishaji na ujifunzaji darasani.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *