Akutwa na misalaba 14 iliyong’olewa makaburini

POLISI mkoani Morogoro inamshikilia fundi seremala, Meshack  Azikam (23) mkazi wa Kata ya Kichangani,Manispaa ya Morogoro kwa tuhuma ya kukutwa na  misalaba 14 ya chuma iliyong’olewa kutoka katika makaburi ya Kola yaliyopo Manispaa ya Morogoro kwa lengo la  kujinufaisha kiuchumi.

Kamanda wa Polisi wa mkoa  huo,  Alex Mkama amesema leo Juni 26, 2023 kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa jana usiku, baada ya kupokea taarifa ya wizi wa misalaba ya chuma katika makaburi hayo.

“ Tumekuwa tukipokea taarifa ya changamoto ya wizi wa misalaba hasa kwa madhehebu ya Kikristu, wamekuja kulalamika na tumefanya ufuatiliaji, “ alisema Mkama na kuongeza kuwa:

“ Katika ufuatiliaji wetu  tulifanikiwa kumkamata mtu mmoja anaitwa  Meshack Azikam (23) fundi seremala mkazi wa Kichangani , Manispaa ya Morogoro ni baada ya kuweka  mtego kwenye  makaburi ya Kola na tukamkamata akiiba  msalaba mmoja,” amesema Kamanda Mkama.

Amesema baada ya kukamatwa na msalaba huo mmoja akiwa makaburini hapo na alienda kupekuliwa nyumbani kwake na alikutwa akiwa na misalaba 14 nyumbani kwake.

“ Mtuhumiwa huyo baada ya kuiba misalaba hiyo anachokifanya ni kuondoa majina ya marehemu na kuipaka upya  rangi na kuiuza tena na kwamba atafikishwa mahakamani wakati wowote ule, “ alisema Kamanda Mkama.

Wakizungumzia tukio la wizi wa misalaba  katika makaburi ya Kola, muumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dayosisi ya Morogoro usharika wa Mji Mpya , Pascal  Mataba ,alisema kuwa suala la wizi wa misalaba inayong’olewa inaonesha wazi watu wamefikia mahali hawana hofu ya Mungu .

Mratibu wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Patrice la Kanisa Katoliki Jimbo la Morogoro , Cosmas Kigona  alisema  msalaba unapowekwa katika  kaburi ni alama  ya utambulisho wa marehemu kwa ndugu zake  wanapokuwa  na shughuli maalumu za kiibada na kuzuru  kaburi lake ,hivyo inapong’olewa ni kupoteza  alama ya mtu huyo alipozikwa.

Habari Zifananazo

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments
Back to top button
0
Would love your thoughts, please comment.x
()
x