Atozwa faini uhujumu miundombinu ya maji

MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga (KUWASA) imemtoza faini ya Sh milioni 2 Samweli Samson Mwita mkazi wa Nyakato kata ya Nyasubi kwa kuhujumu miundombinu ya majisafi kwa kujiunganishia maji na kumwagilia bustani.
Ofisa Uhusiano wa KUWASA, John Mkama amesema Mwita amekubali kosa na kukubali kulipa kulipa kiasi hicho cha fedha kwa awamu mbili ambapo katika awamu ya kwanza amelipa Sh milioni 1.
Sambamba na faini hiyo mamlaka hiyo imeondoa mfumo wote wa huduma ya maji katika makazi ya Samweli hadi atakapomaliza kulipa faini, kisha aanze kuomba upya huduma ya maji.
Aidha mamlaka imemkamata, Hamis Omary mkazi wa Mwime kata ya Mwendakulima kwa tuhuma za kujiunganishia huduma ya maji kwa mtindo wa Bypass katika makazi yake.
Mtendaji wa mtaa wa Mwime, Hussein Hamis ambaye alikuwa shuhuda katika tukio hilo ametoa wito kwa wananchi wa mtaa huo kuacha kuhujuma huduma zinazotolewa na serikali.
KUWASA imeanzisha kampeni ya kuwabaini watu wanaohujumu huduma za maji zinazotolewa kwa umma kwa kushirikiana na wananchi wanaotoa taarifa za siri.