Baada ya tozo Mwigulu atoa maelekezo mapya

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba

MLIPAJI Mkuu wa Serikali ametakiwa kukaa na maofisa masuuli wote kuangalia upya mafungu ya matumizi mengineyo ili miradi ya maendeleo isiathirike baada ya kutangazwa kwa mabadiliko ya tozo za miamala ya kielektroniki.

Maagizo hayo yametolewa leo, Septemba 20, 2022 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba ameagiza matumizi ndani ya serikali yabanwe ili majikumu ya msingi yaweze kutekelezwa.

“Tukate kwenye chai, vitafunwa, misafara kwenye safari za ndani na nje kwa maafisa wa wizara zetu kama Mheshimiwa Rais [Samia Suluhu Hassan] alivyoelekeza, tukate mafunzo, semina, matamasha, warsha,” amesema waziri Mwigulu.

Advertisement

Amesema fedha hizo pia zikatwe kwenye makundi yanayokwenda kukagua mradi mmoja kwa nyakati tofauti au makundi yanayokwenda eneo lilelile kila mtu na gari lake.

“Mfano utakuta wanaenda kwenye eneo moja, wilaya ileile lakini unakuta kila kiongozi na gari lake, kila ofisa na gari lake, tupunguze hii,” ameelekeza.