Bandari ya Karema kuanza kazi leo

Bandari ya Karema

BANDARI ya Karema iliyopo Ziwa Tanganyika inaanza shughuli zake leo baada ya kukamilikwa kwa ujenzi wake uliosimamiwa na  Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).

Kuanza kazi kwa bandari hiyo iliyojengwa kwa Sh bilioni 47.9 kulitangazwa na  Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika,Onesmo Buswelu wakati wa kikao cha wadau akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko.

Alisema uwepo wa bandari hiyo mpya kutafungua ushirikiano mpya wa kibiashara kati ya Tanzania na  majirani zake Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Burundi na Zambia.

Advertisement

Buswelu alitoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa za biashara zinazosababishwa na uwapo wa bandari hiyo.

“Nitoe wito kwa wafanyabiashara na wakulima kutumia bandari mpya iliyojengwa badala ya bandari zisizo rasmi katika Ziwa Tanganyika ili kuiwezesha Serikali kukusanya mapato na kupanga maendeleo yao ipasavyo,” alisema.

Bandari hiyo ambayo ni mradi wa kimkakati ilihusisha ujenzi wa kivunja mawimbi, mlango bandari na gati ya meta 150 zenye uwezo wa kulaza meli zenye urefu wa meta 75 na upana wa meta 15, uchimbaji na uwekaji wa kina wa mlango wa bandari, jengo la ofisi, sebule ya abiria na shehena ya jumla.

Baada ya kukamilika kwa mradi huo bandari hiyo sasa inaweza kuhudumia tani milioni 3 toka tani za awali ambazo ni tani milioni moja.

Akizungumza Kaimu Meneja Mfawidhi wa bandari  za TPA, Ziwa Tanganyika, Edward Mabula alisema lengo la ujenzi wa bandari hiyo ni kutumia fursa kubwa ya soko  ambalo halijafikiwa katika maeneo ya Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Bandari hiyo mpya ya Karema iliyopo  ipo kilomita 123 kutoka Mpanda na kilomita 230 kutoka bandari ya Kigoma na kwamba itaunganishwa na reli ya kisasa ya kisasa (SGR) itakayojengwa  kuanzia Kaliua hadi Bandari ya Karema na hivyo kusaidia  kasi ya usafirishaji wa shehena kwa masoko makubwa kusini – mashariki mwa DRC – Kongo, Zambia na Burundi.

Wabunge wa Majimbo ya Mpanda Vijijini na Mpanda Mjini, Juma Kakoso na Sebastian Kapufi wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema kwamba bandari hiyo ni ufunguo wa uchumi wa mkoa huo na wa taifa la Tanza njia.

 

 

1 comments

Comments are closed.