DODOMA: Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa, amewataka Mameneja wa mikoa wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), kuhakikisha wanaendelea na mapambanona dhidi ya rushwa katika maeneo yao ya kazi na nje ya kazi ili kujenga taswira nzuri kwa Wakala huo na taifa kwa ujumla.
Akizungumza katika kikao kazi kilichowakutanisha Mamemeja hao, tarehe 17 Novemba, jijini Dodoma, Waziri Bashungwa amesisitiza Mameneja hao kuendelea na Mapambano dhidi ya rushwa ni bila kuchoka kwenye sekta ya ujenzi kuanzia manunuzi na usimamizi wa miradi ya ujenzi.
Bashungwa amewata kuhakikisha kuwa wanaripoti kwake au katika mamlaka husika endapo watahisi kuna viashiria vyovyote vya rushwa mapema ili hatua stahiki kuchukuliwa kwa wakati.
“Ninyi ni sehemu ya ulinzi wa kusaidia kupambana na rushwa, msisite kuendelea kupambana na suala hili kwa pamoja kuanzia katika hatua za manunuzi hadi kwenye utekelezaji wa mikataba, amesema Bashungwa
Aidha, Bashungwa amewataka Mamemeneja hao kuhakikisha hatua zinachukuliwa kwa mujibu wa sheria kwa yeyote aliyevamia maeneo ya hifadhi ya barabara na kuendelea kusimamia kwenye maeneo yao kuhakikisha kuwa sheria hiyo haivunjwi.
Bashungwa amewataka Mameneja hao kuwa na tamaduni ya kuwajengea uwezo watumishi wao ili kuongeza ufanisi na tija kwa taasisi hiyo pamoja na Taifa kwa ujumla samambamba na urithishaji wa ujuzi kwa watumishi walio chini yao kwa lengo la kuwekeza katika vizazi vya sasa na vijavyo .
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, amewapongeza Mameneja hao kwa kazi kubwa wanazofanya katika utekelezaji wa miradi mbalimbali nchini na kusisitiza kuendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa viongozi wa serikali waliopo katika maeneo yao.
Naye, Katibu wa Wizara hiyo, Balozi, Mhandisi Aisha Amour, ameishukuru Wizara ya fedha kwa kuendelea kutoa kiasi cha Sh bilioni 70 kila mwezi kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi ambapo kati ya fedha hizo Sh bilioni 20 ni kwa ajili ya wakandarasi wa nje na Sh bilioni 50 ni kwa ajili ya wakandarasi wa ndani.