Biteko acharuka muitikio mdogo Shimmuta

DODOMA: Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati,  Dk. Doto Biteko amemtaka Msajili wa Hazina kufikia Jumanne asubuhi awasilishe maelezo ya kwa nini mashirika mengi ya Umma hayajashiriki Michezo ya SHIMMUTA inayoendelea jijini Dodoma, huku ikitambulika kuwa, mashindano hayo yalianzishwa na Serikali huku mlezi wake akiwa ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ametoa maelekezo hayo jijini Dodoma wakati akifungua Mashindano ya SHIMMUTA yanayohusisha Mashirika ya Umma, Taasisi na Makampuni Binafsi ambapo awali, Mwenyekiti wa Kamati ya SHIMMUTA, Roselyne Massama alimweleza Naibu Waziri Mkuu kuwa wanakumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo ya muitikio mdogo wa Mashirika ya Umma kushiriki mashindano hayo jambo ambalo linazorotesha mashindano hayo.

“‘Viongozi Serikali kama tumekubaliana kufanya jambo fulani basi tulifanye, na kama tunaona halifai  basi bora tuliache, kuliko tunakubaliana kufanya kitu  halafu hatukifanyi, haiwezekani  viongozi wote hapa wanalalamika, Katibu Mkuu analalamika, Naibu Waziri analalamika na mimi nilalamike?, hapana sijaumbwa hivyo, sioni sababu yoyote ya kutamkika au ya kuandikika, kwamba kuna mashirika ya umma 248 na hapa yapo mashirika 57 tu haiwezekani.” Amesisitiza Dk.Biteko

Advertisement

Aidha, amemwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, kuwaandikia barua Makatibu Wakuu wa Wizara ambao Taasisi zao hazijashiriki michezo hiyo, watoe maelezo kwanini hawajapeleka wafanyakazi kwenye mashindano hayo na yeye atashauri viongozi Wakuu wa Nchi, hatua za kuchukua.Vilevile, ameelekeza mashirika yote ya Umma yanayotakiwa kujiunga na SHIMMUTA kufanya hivyo.

 

 

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *