KIGOMA; Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa Kigoma, imekemea tabia ya waendesha pikipiki zinazobeba abiria maarufu kama bodaboda kuendesha pikipiki zao kwa kasi na kuingilia misafara ya viongozi na wakati mwingine kuwa mbele ya misafara hiyo.
Mkuu wa kikosi hicho Wilaya Kigoma, Ibrahim Mbaruku ametoa kauli hiyo wakati wa mkutano wa pamoja baina ya waendesha pikipiki na bajaji na maofisa wa Mamlaka ya Mapato (TRA) Mkoa Kigoma, mkutano uliokuwa ukitoa elimu na ufafanuzi wa sheria mpya ya kodi ya mapato ambayo waendesha pikipiki hao wataanza kulipa.
Amesema bodaboda hao wamekuwa wakiingilia misafara ya mawaziri, mkuu wa mkoa na misafara mingine ya viongozi, huku wakiwa hawachukui hatua zozote za tahadhari kujiepusha na kuwaepusha watumiaji wengine wa barabara na ajali ambazo zinaweza kutokea.

Kutokana na hali hiyo amesema kuwa polisi imejizatiti kuhakikisha inawashughulikia bodaboda wasiofuata sheria na taratibu za usalama barabarani, ikiwemo pia tabia ya kubeba mishikaki, kutovaa helmet, kung’oa vioo vya pembeni na kuweka majina yao kwenye namba ya usajili bila kufuata taratibu.

Akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa Wilaya Kigoma, Salum Kali amesema bodaboda ni kundi muhimu katika maendeleo ya taifa, lakini vitendo wanavyofanya hasa kwenye kukiuka masuala ya ulinzi na usalama hasa wakati huu, ambapo taarifa zinaonesha kuwa kundi hilo linahusika kwa kiasi kikubwa na vitendo vya uporaji hasa nyakati za usiku.