BRELA waombwa kusaidia wafanyabiashara Mara

BRELA waombwa kusaidia wafanyabiashara Mara

RAIS wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA),  Paul Koy, ameishauri Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), kusaidia wafanyabiashara wa Mkoa Mara, ili warasimishe biashara zao.

Kauli hiyo ameitoa alipotembelea banda la BRELA kwenye maonesho ya Mara Business Expo 2022, yanayofanyika Musoma,  mkoani Mara.

“Nawaomba sana BRELA muwasaidie wafanyabiashara wa mkoa huu, maana wanahitaji sana huduma zenu,” amesema.

Advertisement

Amesema mbali na kutoa huduma za usajili na utoaji wa leseni kwenye banda, inabidi BRELA itoe elimu kwa wananchi wanaozalisha bidhaa mbalimbali.

Kwa upande  wake Ofisa Leseni wa BRELA,  Rajab Chambega, amemhakikishia kuwa taasisi hiyo imejipanga vyema kutoa huduma kwa wafanyabiashara Mkoa wa Mara na mikoa jirani wanaotembelea maonesho hayo.

BRELA inashiriki kwenye Maonesho ya Mara Business Expo 2022 na kutoa huduma za usajili na utoaji wa leseni papo kwa hapo, hadi  Septemba 11, 2022.