CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeahidi kushirikiana na chama cha Ukombozi wa Msumbiji, FRELIMO pamoja va vingine vyenye mrengo kama huo.
Mwenyekiti wa CCM Taifa ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewaahidi hayo katika kongamano la 12 wa Frelimo huko Maputo, Msumbiji leo, Ijumaa huku akisisitiza vyama hivyo vinapaswa kuendelea kushirikiana kwani kinyume chake, vitakufa.
Amesema vyama hivyo vina jukumu la kuendelea kudumisha amani na utulivu katika nchi zao na katika ukanda wote wa kusini.
“Je, tunatakiwa tuache vyama vyetu vife? Alihoji na kuongeza: “Sasa ili tuendelee kudumu madarakani lazima tuje na fikra mpya, tujifunze kwa vyama vilivyoondolewa madarakani…amani na utulivu ni matokeo ya vyama vyetu kuendelea kuwepo madarakani, vikiondolewa hakutakuwa na amani.
”
Aidha, amesema wapigania uhuru wa Msumbiji kupitia Frelimo na vyama vingine ya ukombozi vya nchi za kusini mwa Afrika vilitumia ardhi ya Tanzania katika kuendesha mapambano dhidi ya tawala za kikoloni nchini mwao.
“Wapigania uhuru watakumbuka maeneo ya Kongwa na Dakawa kwa kuwa yalitumika kuwafunza na kuweka mikakati ya kupambana na ukoloni wa Wareno, maeneo haya pia yalitumiwa na NPLA ya Angola, ZANU PF ya Zimbabwe, SWAPO ya Namibia na ANC ya Afrika Kusini, historia hii ya undugu na ushirikiano miongoni mwa vyama hivi sita imesaidia pia kuimarisha uhusiano baina ya watu wetu,”amesema.