Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga, kimesema hakitamvumilia mwanasiasa yeyote ndani ya chama hicho ambaye atafanya siasa za vurugu ikiwemo zinazokashifu mazuri yanayofanywa na serikali.
Angalizo hilo limetolewa leo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa Rajab Abdallah, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Tanga na kuwataka viongozi hao wa siasa kutumia ruhusa ya mikutano ya hadhara kufanya siasa zenye tija na maendeleo.
“CCM haitamvumila mwanasiasa au kiongozi ambaye atafanya siasa za vurugu tutashughulika naye kweli, “amesema Mwenyekiti huyo.
Amesema kuwa chama hicho kimejipanga kufanya mikutano ya mfano ambayo inalenga kueleza mazuri ambayo serikali ya awamu ya sita imeyafanya, ikiwemo kuhamasisha umoja na mshikamano miongoni mwa mwananchi na viongozi wao.
Hata hivyo Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mohamed Ratco, amewataka viongozi wa vyama upinzani kutotumia uhuru wa mikutano ya hadhara vibaya Kwa kufanya siasa zenye kuleta vurugu.