Chadema yatangaza kuzindua mikutano ya hadhara

KAMATI Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imetangaza uzinduzi rasmi wa mikutano ya hadhara kitaifa ya chama hicho itakayoanza Januari 21, mwaka huu.

Aidha, chama hicho kimesema kimeridhishwa na mwenendo wa mazungumzo ya maridhiano baina ya timu ya Chadema inayoongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe na timu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inayoongozwa na Makamu Mwenyekiti, Abdulrahman Kinana.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Mawasiliano, Itifaki na Mambo ya Nje ya Chadema, John Mrema, uzinduzi rasmi wa mikutano ya hadhara kitaifa utafanyika Januari 21, mwaka huu na kufuatiwa na uzinduzi wa mikutano kama hiyo kwenye kila makao makuu ya kanda.

Advertisement

Chama kimetangaza uamuzi huo ikiwa ni siku nne tangu Rais Samia Suluhu Hassan alipoondoa zuio la mikutano ya hadhara wakati akizungumza Ikulu, Dar es Salaam na viongozi wa vyama 19 vya siasa vyenye usajili wa kudumu.

Rais Samia alivitaka vyama na wanasiasa kufuata sheria, kanuni na miongozo wakati wa kufanya mikutano hiyo na kuepuka kutumia uhuru wa demokrasia  vibaya kwa sababu sheria itachukua mkondo wake.

/* */