Chalamila aibua rushwa mpya vizuizi Kagera

Chalamila aibua rushwa mpya vizuizi Kagera

UTITIRI wa vizuizi vya ukaguzi  (beria), imeelezwa ni chanzo kikuu cha rushwa mkoani Kagera, ambapo mtumishi mmoja ndani ya saa tatu anachukua rushwa ya Sh 960,000, ikiwa ni  wastani wa  Sh  320,000 kwa saa.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Albert Chalamila katika Mkutano wa Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Abdulrahman Kinana ambae yupo mkoani Kagera kukagua miradi ya serikali na uhai wa chama.

Chalamila amesema baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), wanaohudumu vituo hivyo wamekuwa sio waaminifu wanavitumia  vibaya kwa kutoza faini za juu kwa  wasafirishaji,  jambo ambalo humlazimu mtozwa faini kutafuta mbadala wa kukwepa faini, hivyo kujengeka mazingira ya rushwa kirahisi.

Advertisement

“Mheshimiwa  Makamu Mwenyekiti (Kinana),  Mkoa huu una utitiri wa beria na ni chanzo kikuu cha ‘mchwa’, wanakamata vitu vya watu mpaka mikungu ya ndizi, kesho yake ukienda haipo.

“Maduka mengi ya Watanzania Mtukula yapo upande wa Uganda, huku upande wa Tanzania  hamna, leo hii saa tatu na nusu  kuna mtumishi amechukua rushwa ya shilingi 960,000  kwa maana nyingine mtu huyo amechukua 320,000 kwa kila saa moja, ndani ya saa tatu kashakusanya kiasi hicho cha fedha.

“Wapo 14,   Jumatatu mtapata majibu yao…..wanatengeneza  mazingira magumu kwa wafanyabiashara, ili tu wapate rushwa,” amesema.

Amesema tayari ameshaanza kuchukua hatua kwa kuunda kamati ndogo na baadhi ya beria zitapunguzwa.

Kauli ya Chalamila imekuja kufuatia malalamiko mengi yaliyotolewa na wafanyabiashara kwa Kinana, ambaye alitaka kujua changamoto zinazowakabili wafanyabiashara wa mkoa huo.

Katika mkutano huo, wafanyabiashara hao  walilalamikia utitiri wa beria zilizopo barabarani, unapoingia na kutoka Tanzania kupitia mpaka wa Uganda, eneo la Mtukula.

Eneo lilalolalamikiwa zaidi ni kutokea Mtukula hadi Bukoba mjini ambapo kuna wingi wa vituo njiani.

Mmoja wa wafanyabiashara hao, Jane Charles alisema kutokea  Mtukula hadi Bukoba Mjini kuna beria zaidi ya tisa  upande wa Tanzania, lakini ukiingia Uganda hadi mjini kuna beria moja…na kibaya zaidi ukiangalia beria hizo nyingine zinafanya kazi sawa na beria zingine na kudai kuwa ni usumbufu kwa wafanyabiashara.

Kwa upande wa Kinana akizungumzia hilo alisema: “Hata mimi nimeziona beria  ni nyingi, nikipita zinafunguliwa, nikivuka zinafungwa,  mtu gunia moja anaulizwa kodi, hata kuuza hajauza, sisemi msikate tozo ila ziwe rafiki.”

Amesema atakutana na wabunge wote wa mikoa ya mipakani Kilimanjaro, Katavi, Kagera, Kigoma, Mbeya na  kuzungumza nao ili hatua zaidi kuchukuliwa.