SERIKALI imetangaza kumfuta jasho kwa kumpatia kitita cha sh milioni 10 daktari aliyepata changamoto ya kiafya wakati akiwa kwenye mapambano dhidi ya milipuko wa ugonjwa wa virusi vya Marburg uliotokea mkoani Kagera mwezi Machi mwaka huu.
Hayo yamesemwa na Naibu waziri wa Afya Godwin Moleli katika kikao kazi na wahudumu wa sekta ya afya katika mkoani huo
” Nawapongeza wahudumu wetu wa afya kwa kazi kubwa mliyoifanya ya kupambana na ugonjwa huu, hali ilikuwa ya hatari na ngumu lakini mlipambana mno hivyo pokeeni shukrani zetu za dhati,”amesema Mollel.
Amesema, katika mapambano dhidi ya ugonjwa huyo kuna daktari aliyepata changamoto ya kiafya serikali haiwezi kumuacha hivyo amemuagiza Mganga Mkuu wa Mkoa huo Dk Isesanda Kaniki kumpa kiasi cha shilingi milioni 10 ili ziweze kumsaidia katika kipindi hiki kugumu.
“Huyu ni Kama mwanajeshi aliyejeruhiwa vitani hivyo hatuwezi kumuacha kabisa,”amesema.a
Nae, Dk Kaniki akizungumza amesema daktari huyo alipewa shilingi milioni 2 na amelipiwa kodi ya nyumba kwa muda wa mwaka mzima na amepewa samani mbalimbali ambazo anazitumia.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa Afya Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Ntuli Kapologwe amemshukuru Naibu waziri wa Afya kwa motisha hiyo kwa daktari huyo aliyeathirika kwa Marburg kwani kwa kufanya hivyo amewapa ari watumishi kuzidi kufanya kazi kwa bidii.
Aidha, Dkt.Kapologwe amewasa watumishi katika sekta ya afya kutunza rasilimali zinazotolewa na serikali pamoja na wadau ili thamani ya fedha iweze kuonekana kwa wananchi.