DODOMA: DAR ES SALAAM ni Jiji kubwa, la kibiashara na mboni ya taifa, hekaheka zake ni kama sherehe za Krismasi au Eid.
Hayo yamesemwa leo bungeni jijini Dodoma Mei 09, 2024 na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ambapo amesisitiza kuwa wizara hiyo ipo macho kuhakikisha Jiji la Dar es Salaam linapata maji ya uhakika.

“Waheshimiwa wa Majimbo yanayohudumiwa na DAWASA (Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam) asanteni sana kwa ushirikiano wenu,” amesema Aweso.
Aweso amezungumzia mradi wa kihistoria wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda ambalo ni la miaka mingi tangu miaka ya 1950.
“Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere amelikuta na ameliendeleza, baada ya miaka zaidi ya 60, Mama Samia anajenga Bwawa la Kidunda tena kwa fedha za ndani. Chezea Mama Samia wewe, hakika hii inadhihirisha umuhimu wa kipindi cha TV cha Songa na Samia cha Zuhura Yunus. Songa na Samia, Songa na Samia, Songa na Samia,” amesisitiza na kuongeza
“Bwawa hili ni muarobaini wa shida ya maji katika Majimbo ya Chalinze, Bagamoyo, Kibamba, Ubungo, Kawe, Kinondoni, Ilala, Kigamboni, Segerea, Ukonga, Kisarawe, Mkuranga, Mbagala, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini, na sehemu za Handeni na Morogoro Vijijini. Waheshimiwa Wabunge, mambo yako bambam, bambam, bambam sana,” amesema Aweso
Soma pia: https://habarileo.co.tz/rais-samia-azindua-mradi-wa-maji-kigamboni/
Aidha, amesema serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo imeendelea kujenga, kukarabati na kupanua miundombinu ya majisafi na usafi wa mazingira katika maeneo ya mijini.
“Katika mwaka 2023/24, jumla ya miradi 244 ilipangwa kutekelezwa ambapo hadi mwezi Aprili 2024, miradi 85 imekamilika na miradi 159 ipo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji.
Utekelezaji wa baadhi ya miradi ya majisafi na usafi wa mazingira katika Miji Mikuu ya Mikoa, Miji Mikuu ya Wilaya, Miji Midogo, na Miradi ya Kitaifa”
“Wizara imeanza kujenga mtandao wa usambazaji maji na matanki ya kuhifadhi maji Kusini mwa Dar es Salaam kwa gharama ya Shilingi bilioni 35.15. Hadi mwezi Aprili 2024, utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 19 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2024 na kunufaisha wakazi wapatao 450,00,” amesema.
Tazama: https://www.youtube.com/watch?v=BMckMA5tHkg
Aidha amesema “Wizara imeendelea kutekeleza mipango ya muda mfupi inayolenga kukabiliana na adha ya upatikanaji wa maji katika Jiji la Dodoma ambapo hadi mwezi Aprili 2024, Wizara imekamilisha utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi wa ujenzi na uboreshaji wa mtandao wa majisafi Nzuguni unaohudumia wakazi 75,968 wa maeneo ya Nzuguni, Ilazo, Swaswa na Kisasa. Aidha, awamu ya pili ya mradi imeanza kwa gharama ya Shilingi bilioni 5.51 na utanufaisha wakazi wapatao 80,000.
”
Amesema, kwa upande wa huduma ya maji katika Jiji la Arusha ni ya uhakika na hivyo inalinda na kulipa hadhi Jiji la Arusha ambalo ni kitovu cha utalii nchini. Huduma ya Maji Arusha inapeperusha agenda ya Royal Tour, Agenda ya Mheshimiwa Rais Mama Samia, ” amesema.