David Malisa azindua msimu wa 5 Hello Mr Rights

MKURUGENZI wa Masoko na Maudhui wa Startimes David Malisa amezindua msimu wa tano wa onesho la Hello Mr Rights maalum kwa ajili ya kutafutia vijana wenza wa maisha.
Akizungumza Dar es Salaam leo kwenye uzinduzi wa onesho hilo, Malisa alisema wanajivunia kuona tangu wameanza kuna vijana wengi wamenufaika kwa kupata watu sahihi wa maisha na kadiri miaka inavyosogea wamekuwa wakipata maombi ya vijana kutaka kushiriki.
Amesema sio tu vijana bali kuna mastaa kibao wamekuwa wakituma maombi kuomba ushiriki wao kwenye onesho hilo linalorushwa kupitia Chanel ya St Bongo.
“Mtakubaliana na mimi kwamba shoo hii imeweza kukua kwa kasi sana na kupata umaarufu mkubwa kwa kuongeza idadi ya mashabiki kila msimu na msimu huu unakuja na maboresho mengi makubwa zaidi ili kuongeza ladha ya burudani kwa kila mtazamaji,” amesema na kuongeza:
“Visimbuzi vyetu tumevishusha bei kupitia kampeni ya Lipa Tukubusti ni fursa kwako mtazamaji kuchangamkia ili kufurahia burudani hii.”
Mkuu wa Usimamizi wa Chanel ya St Bongo, Shikunzi Haonga amesema onesho hilo litaanza kurushwa kwenye chanel hiyo kuanzia Desemba mosi mwaka huu.
Mwendeshaji wa kipindi hicho Godfrey Rugarabamu ‘MC Gara B’, amesema vijana zaidi ya 30 watakaoshiriki katika onesho hilo watapewa elimu ya mahusiano, elimu ya afya na mambo mbalimbali ya maisha.
Amesema msimu huu utakuwa na ‘surprise’ nyingi ikiwemo kuwaonesha vijana waliofanikiwa kupata wenza kupitia kipindi hicho kama bado wako kwenye mahusiano, ndoa lakini pia, kujua changamoto na mafanikio yao.
Meneja Masoko wa St Bongo, Magreth Lawrence ameomba wafanyabiashara na kampuni kuwaunga mkono kwa kudhamini onesho hilo.