DAR ES SALAAM: BAADA ya msanii wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platinumz kuonyesha nia ya kuimba wimbo katika albamu ya msanii wa singeli Sholo Mwamba, msanii huyo amemjibu Diamond kwamba yupo tayari na hiyo ni moja ya ndoto zake lakini ndoto hiyo itakamilika watakapofanikisha kurekodi wimbo huo.
Diamond Platinumz ametamani kuimba na Sholo Mwamba baada ya Sholo kutangaza jina la albamu yake ‘Another Boy from Tandale’ likifanana na jina la albamu ya kwanza ya Diamond aliyoiita ‘A Boy from Tandale’.
Sholo amesema wimbo wake na Diamond ukifanikiwa kurekodiwa utampa neno la kusema huku akiamini atakuwa ametoa kiu ya mashabiki wake waliotamani afanye hivyo muda mrefu.
“Mashabiki wangu waliniomba niimbe na Diamond muda mrefu lakini haikufanikiwa sasa wakati ndiyo huu kama alivyotaka mwenyewe mimi nimekubali ninaimani tutarekodi katika kiwango cha juu sana na wimbo utafika mbali,” amesema Sholo Mwamba.
Akizungumzia jina hilo la another boy from tandale amesema limekuja baada ya kuona mafanikio ya Diamond aliyekuwa akiishi Tandale na mafanikio yake ya kimuziki yamewabadilisha vijana wengi waliokuwa na maisha na tabia zisizofaa kwa jamii akiwemo yeye.
“Diamond ametubadilisha mno vijana wa Tandale ambao kipindi kile kama hukuwa mwizi utakuwa mtumia dawa za kulevya (teja),” ameeleza Sholo Mwamba.