DAR ES SALAAM: MUONGOZAJI maarufu wa video za wasanii ndani na nje ya nchi, Ivan Peter maarufu Director Ivan amesema ili director adumu na wasanii wengi katika kazi yake lazima awe anatunza siri za wasanii anaofanya nao kazi.
Amesema waongozaji na wasanii wengi wanashindwa kuwa na siri za video zao hivyo kusababisha video kuvuja.
Director Ivan aliyeandaa video ya wimbo ‘I Made it’ wa Harmonize uliogharimu zaidi ya Sh milion 135 amesema siri kubwa ya kufanya kazi na wasanii wengi ni kutunza siri za wasanii usivujishe video ulizowafanyia.
“Mimi nilijitafuta tangu muda mrefu niliamua kufanya kazi na wasanii wote bila kubagua na huwa natunza siri za wasani katika kazi zao na kuhakisha hazivuji hadi watakapoamua kuziachia wao wenyewe,” amesema Ivan.
Ivan amesema wasanii wanatakiwa wawekeze kwenye wimbo na video na wakubali kwamba mambo yamebadilika huku akisisitiza ni lazima kuwa na uwekezaji mkubwa wa fedha.