Dk Biteko: REA pelekeni huduma vijijini

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk Dotto Biteko ameagiza watendaji wa Wakala wa Umeme Vijijini (REA) kujikita zaidi kufanya kazi vijijini badala ya kuwekeza muda mwingi wakifanya vikao mjini.

Dk Biteko ametoa maelekezo hayo baada ya kuwasha umeme katika kijiji cha Ihako kata ya Katome wilayani Bukombe mkoani Geita ikiwa ni sehemu ya mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili.

Amesema REA wanapaswa kujikita vijijini wanapotathimini, kusimamia na kutekeleza miradi ya umeme ili kung’amua na kushughulikia changamoto zilizopo na kuboresha huduma za nishati ya umeme nchini.

Advertisement

“Nyie ni wakala wa umeme vijijini, siyo wakala wa umeme mijini, vikao vyenu tuwaone mna wananchi, tuone magari yenu yanapita humu wanamopita wananchi, wenye maisha ya kawaida, muende huko,”

“Mkajifunze lugha yao, mjue shida yao, sasa hivi tunataka nishati ya kupikia, watu wanaohangaika na nishati ya kupikia kwa kiasi kikubwa ni wanannchi hawa wa hali ya chini, hawa ndio tushughulike nao.”

Ameahidi serikali imepanga kufikisha umeme kwa watanzania wote pasipo kubagua thamani ya nyumba zao huku akiwataka watanzania kuendelea kuvumilia kwani wizara yake inashughulikia tatizo la mgawo wa umeme.

Mkurugenzi Mkuu REA, Mhandisi Hassan Saidy amesema kijiji cha Ihako ni miongoni mwa vijiji 127 mkoani Geita vitakavyowashiwa umeme ambapo ni sehemu ya vijiji 4,071 vilivyopo kwenye mradi nchi nzima.

Amesema, mwaka huu wa fedha wametenga kiasi cha Sh bilioni 21 kutekeleza mradi wa ujazilizi awamu ya pili B, kufikisha umeme kwenye maeneo 137 na pia kuanza kupeleka umeme kwenye vitongoji 105.

Amebainisha katika REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili, tayari vijiji 2,740 vimeshaunganishiwa umeme na kazi inaendelea dhamira ikiwa ni kukamilisha umeme kwenye vijiji vyote 12,318 vya Tanzania bara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Lutengani Mwalwiba amesema kuwasha umeme katika kata ya Ihako itaboresha utendaji wa shughuli za kiserikali kwenye shule na ofisi za umma.

“Walimu walikuwa wanalazimika kusafiri umbali mkubwa zaidi ya kilomita 25 mpaka kule Ushirombo ili waweze kufanya kazi, lakini kama umeme umekuja kazi hizi zinaenda kufanyika kwa wepesi zaidi.”

Mwenyekiti wa kijiji cha Ihako kata ya Katome, Nzalia Masayi amesema kijiji chake kina wakazi takribani 500 watakaonufaika na umeme kutokea vitongoji vinne, na hadi sasa kaya 60 zimeunganishiwa umeme.

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *