MAKAMU wa Rais, Dk Philip Mpango amehimiza wananchi kutobaguana kwa itikadi za kisiasa wakati wa changamoto mbalimbali ikiwemo msiba unapotokea katika jamii.
Alisema hayo wakati akiwafariji wafiwa na waombolezaji waliojitokeza katika ibada ya kuaga mwili wa marehemu Midlaster Nsanzugwako ambaye ni mke wa aliyekuwa Mbunge wa Kasulu Mjini, Daniel Nsanzugwako iliyofanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Bethel – Kasulu, mkoani Kigoma jana.
Dk Mpango alisema ni muhimu kushikamana vema changamoto zinapojitokeza. Alisisitiza pia jamii kutenga muda kwa ajili ya kumuomba Mungu wakati wote wa maisha, licha ya majukumu na kazi zilizopo.
Aliwaasa wananchi hao kujifunza kutumikia wengine katika jamii kama ilivyokuwa kwa Midlaster. Nsanzugwako. Viongozi wengine waliohudhuria ibada hiyo ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Thobias Andengenye, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kigoma, Jamal Tamim.
Comments are closed.