BARAZA La Biashara Afrika Mashariki (EABC), limewateua Watanzania watatu kuwa mabalozi wa baraza hilo nchini.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), uteuzi huo unalenga kuhakikisha baraza hilo linatimiza wajibu wake ipasavyo na kufanya biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na nchi za Afrika Mashariki bila vikwazo.
Walioteuliwa ni Mtaalam wa Diplomasia ya Uchumi TPSF, Raphael Maganga, Mwenyekiti wa Tanzania Women Chamber of Commerce, Mercy Sila na Mkurugenzi Mtendaji Daima Associates, Samuel Nyantahe.
EABC iliundwa 1998, kama kiungo muhimu katika mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao ulisisitiza ushiriki wa sekta binafsi, ili kufikia maendeleo endelevu ya kijamii, kiuchumi na kisiasa.
Baraza hilo ndio mwamvuli wa vyama vyote vya biashara katika nchi zote saba za Jumuiya ya Afrika Mashariki.