WAWAKILISHI wa taasisi mbalimbali za ubunifu wa teknolojia katika Jimbo la Washington nchini Marekani wamefurahishwa na uzuri wa Tanzania mara baada ya kupata fursa ya kutazama sehemu ya filamu ya Tanzania; ‘The Royal Tour.”
Wawakilishi hao wakiongozwa na mmiliki wa klabu ya Ligi Kuu ya Mpira wa Miguu ya Marekani na mabingwa wa Mabara, Seattle Sounders, Adrian Hanauer, ambaye pia ni mwanahisa katika kampuni kubwa ya Amazon, walionekana wakishangilia na kupiga makofi katika sehemu mbalimbali za filamu hiyo huku wengi wakiahidi kuwa Julai mwaka huu watatembelea Tanzania.
“Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ni mwanamke wa kwanza katika historia ya nchi yetu kushika wadhifa huo, amejitoa kuwa kama mwongoza watalii na kuionesha nchi yetu kazika filamu hii ya Royal Tour katika namna ambayo haijawahi kutokea.
“Amesema Damas Mfugale Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB).
Mbali mmiliki wa klabu ya Seattle Sounders, baadhi ya wawakilishi wa taasisi nyingine kubwa na za kimkakati waliohudhuria hafla hiyo na kuitazama filamu ya Royal Tour ilioneshwa kupitia skrini kubwa za uwanja wa Lumen moja ya viwanja vitakavyotumika pia kwa fainali za Kombe la Dunia 2026 ni David Young, Afisa Mwendeshaji Mkuu wa Klabu ya Seattle Seahawks, Andrea Bailey kutoka klabu ya NBA ya Portland Trail Blazers.
Wengine ni Michael Woody, kutoka kampuni ya Visit Seattle, Anbessie Yitbarek, Makamu wa Rais wa Masuala ya Biashara Ukanda wa Afrika kutoka kampuni ya Boeing, Reed Forrester Meneja Shirika la Ndege la Delta, AJ Jones II, Afisa Mwandamizi wa Mawasiliano, kampuni ya Starbucks na Sarah Gavin, kutoka makao makuu ya Google.