Gary Cahill atangaza kustaafu soka

BEKI wa zamani wa timu ya Taifa ya Uingereza na Chelsea, Gary Cahill ametangaza kustaafu kucheza soka akiwa na umri wa miaka 36.
Cahill, ambaye alicheza mechi 61 na kuifungia nchi yake mabao matano, amekuwa hana timu tangu alipoondoka Bournemouth majira ya joto.
Mshindi huyo mara mbili wa Ligi Kuu ya England anaamini sasa ni wakati wa kutundika daruga.
“Nimekuwa na uamuzi mgumu katika baadhi ya vipengele lakini nadhani nilijua tu kwamba safari lazima iwe na mwisho katika hatua fulani.
Nilipata hisia kwamba sasa ni wakati mwafaka.”amesema Cahil.
Cahill aliingia katika kikosi cha England alipokuwa Bolton Wanderers, na kucheza mechi yake ya kwanza dhidi ya Bulgaria katika ushindi wa 4-0 Septemba 2010. Kwa kufanya hivyo, akawa mchezaji wa kwanza wa Bolton kuichezea England tangu alipofanya hivyo Michael Ricketts mwaka wa 2002.