Geita waja kivingine ukusanyaji taka

HALMASHAURI ya Mji wa Geita mkoani hapa imeanza kutekeleza mradi wa maboresho ya ukusanyaji, uhifadhi na  uchakataji wa taka, ili kuimarisha usafi wa mazingira na kuongeza mapato kupitia taka.

Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti wa Taka na Usafi wa Mazingira Halmashauri ya Mji wa Geita, Aloys Mutayuga ameeleza hayo leo katika mahojiano maalum na HabariLEO.

Amesema hatua hiyo imeanza kwa kusambaza makontena matano ya kuhifadhi taka kwa kila kituo, kwenye vituo 10 mjini Geita ili kutoa fursa kwa watupa taka kutenganisha taka na kurahisha uchakataji.

“Tumeanza na makotena 50, na hizo kontena 50 kila moja kuanzia kuisafirisha na kuiweka hapo ilipo imegharimu shilingi milioni 1.7, kwa hiyo hizo kontena 50 zimegharimu jumla ya Shilingi milioni 85.

“Tunayaweka kando ya barabara kwa sababu kuna watu wanatembea wanakula, wanakunywa maji, wanabeba taka tofauti wanatupa kwenye mtaro, sasa hivi tunataka kudhibiti utupaji taka hovyo,” amesema.

Ameeleza utenganishaji wa taka utafanikisha mradi wa halmashauri wa taka kuzifanyia urejeshaji (recycling) kwa kuzalisha mbolea kutoka taka ozo, kuzalisha mkaa kwa makaratasi na taka za plastiki zitauzwa viwandani.

Amesema hadi sasa halmashauri ina uwezo wa kukusanya tani 2800 kati ya tani 5700 za taka inayozalishwa kwa mwezi sawa na ufanisi wa asilimia 49, huku lengo ni kufikia ufanisi wa asilimia 60 mwaka wa fedha 2023/24.

Amesema ufanisi utaongezeka kwa kuongeza vikusanya taka kwani kwa sasa wana magari madogo mawili, matrekta matatu na  gari kubwa moja lililotolewa kwa ufadhili wa Kuwait na hivo wataongeza matrekita matatu.

Amesema mipango hiyo itachagiza usimamizi thabiti wa sheria ndogo ya usafi wa mazingira ya halmashauri ya mji toleo namba 269 ya Oktoba 19, 2018 inayoelekeza usafi wa mazingira.

“Usingeweza kumtoza mtu faini kabla ya kuweka miundombinu ambayo inasaidia kile kitu unachotaka kifanyike, kwa hiyo sisi kama halmashauri tumeweka hayo makasha kinachofuata kusimamia sheria.

“Ni jukumu la wananchi kujua kama nina chupa ya maji, kama nina mabaki ya vyakula nikaweke pale, ukitupa hovyo wakikukamata wasimamizi wa kamati  ya mazingira ya mitaa ni halali yao.”

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita, Zahra Michuzi amesema wamejipanga kutenga bajeti ya kutosha kuhakikisha mradi wa uchakataji taka unakuwa endelevu, ili kuimarisha usafi wa mji na kuongeza mapato kila mwaka.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button