Giniki, Sakillu wang’ara tamasha la Karatu

EMMANUEL Giniki na Jackline Sakillu wameng’ara katika msimu wa 21 wa Tamasha la Michezo na Utamaduni la Karatu baada ya kushika nafasi za kwanza katika mbio za wanaume na wanawake mjini hapa jana.

Mbali na hao, wapanda baiskeli wa Shinyanga nao walitamba katika tamasha hilo katika mbio za baiskeli za kilometa 60 baada ya kushika nafasi nne za kwanza huku  wakiwaacha Arusha wakiambulia nafasi ya tano.

Giniki kutoka klabu ya Talent ya Arusha alimaliza wa kwanza katika mbio za kilometa 10 kwa wanaume akitumia dakika 30:01.82 akifuatiwa na Inyasi Sulle naye wa Talent aliyetumia dakika 30:30.01 huku Josephat Bitemo wa Polisi akimaliza watatu kwa kutumia dakika 31:11.54.

Advertisement

Sakilu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) alimaliza wa kwanza katika mbio za kilome tano kwa wanawake alipotumia dakika 15:20.91 wakati mwanariadha chipukizi kutoka Serengeti, Neema Nyaisawa alimaliza wa pili kwa kutumia dakika 15:41.19 na Agness Protas wa JWTZ alimaliza watatu kwa dakika 15:52.19.

Katika mchezo wa baiskeli, Richard Charles, Mashanga Dura, Paulo Mihambo na Lameck Shiwelu wote wa Shinyanga walishika nafasi nne za kwanza kwa kutumia saa 1:48.09.22, 1:48.13.66, 1:48.16.35 na 1:50.49.10, huku nafasi ya tano ikienda Arusha kwa Mussa Hussein aliyetumia saa .1:50.50.10.

Kwa upande wa baiskeli wanawake wa Shinyanga nao walitamba baada ya kushika nafasi zote za juu.

Giniki alisema kuwa mbio zilikuwa ngumu hasa kutokana na joto na njia kuwa na milima na ushindani kutoka kwa wanariadha wengine walioshiriki mbio hizo za kila mwaka, ambazo hufanyika Desemba.

Mbali na riadha na baiskeli pia tamasha hilo lilihusisha mpira wa wavu, soka, ngoma, sarakasi na kwaya kutoka vikundi mbalimbali vya sanaa, ambavyo vilikonga nyoyo za mashabiki waliojitokeza kushuhudia tamasha hilo katika viwanja vya Mazingira Bora mjini hapa.

1 comments

Comments are closed.

/* */