MKUU wa mkoa wa Mtwara Gelasius Byakanwa amewataka viongozi wa halmashauri zote mkaoni hapa kuweka mipango mikakati ya kuhakikisha kila Kata inakuwa na shule ya sekondari ili kuwaondolea wanafunzi adha ya kutembea umbali mrefu kufuata masomo ambapo kata 58 zikiwa hazina shule za sekondari kati ya kata 191 zilizopo mkoani humo.
Agizo hilo limetolewa na mkuu wa mkoa huyo wa Mtwara wakati wa Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) mwaka 2021 kilichofanyika mkoani humo ambapo taarifa mbalimbali zimewasilishwa kwenye kikao hicho ikiwemo hiyo ya elimu.
Alisema kuwa kumekuwa na baadhi ya kata mkoani humo kutotimiza agizo la serikali kwamba kila kata iwe na shule ya sekondari na matokeo yake wilaya inabaki haina vyumba vya madarasa hatimaye wanafunzi wanatembea umbali marefu kufuata elimu.
"Tatizo la wilaya fulani kutokuwa na vyumba vya madarasa kunatokana na kutotimiza agizo hili la serikali, kama tutaweza kusimama tukahakikisha kila kata inakuwa na vyumba vya madarasa kwani kila kata itakuwa inajitegemea na wanafunzi hawatakuwa wanatembea umbali mrefu kwenda shule badala yake watatembea umbali mfupi kufika kwenye eneo la shule,” alisema Byakanwa.
Hata hivyo mkuu wa mkoa huyo wa mkoa amezungumzia tatizo la uhaba wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari mkoani humo pamoja na kwamba kwa sekondari uhaba huo inawezekana ikawa unatokana na sulala la ongezeko la udahili wa wanafunzi kutoka darasa la saba kwenda sekondari.
Ofisa elimu mkoa wa Mtwara, Kiduma Mageni alisema kuwa watahiniwa wote 22,316 waliofaulu mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2020 walifanikiwa kuchaguliwa kidato cha kwanza mwaka 2021 kati yao wakiwemo wavulana 10,882 na wasichana 11,434.