Hakuna nyaraka sahihi malipo Sh Bil 1.95 Tanapa

MAMLAKA ya Hifadhi ya Taifa (TANAPA), imefanya malipo mbalimbali yenye thamani ya Sh bilioni 1.95 kupitia hati za malipo 40 zilizokosa uhalali wa malipo na kutothitibishwa kutokana na kukosekana kwa nyaraka sahihi za viambatisho licha ya kuorodheshwa majina ya waliolipwa. Ripoti ya CAG imeeleza.
–
Akizungumza wakati wa uwasilishaji wa ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Mkuu wa Hesabu za Serikali, CAG Charles Kichere amesema mbali na hilo Sh bilioni 1.34 zilionesha kupokelewa na watumishi mbalimbali kupitia hati za malipo zilizosainiwa huku milioni 611 zikishindwa kuthibitishwa kupokelewa na watumishi husika.
–
“Lakini pia nilibaini kiasi cha posho kilicholipwa zaidi na juu ya viwango vilivyoidhinishwa cha Sh milioni 38.72 kinyume na miongozo,” amesema CAG Kichere.
–
CAG Kichere amesema Sh milioni 114 zililipwa mara mbili kwa shughuli moja ya uandaaji wa hesabu.
–
Amependekeza kuwa Menejimenti ya Uhifadhi ya Taifa Tanzania kuhakikisha fedha hizo zinarejeshwa na kuhakikisha udhibiti wa malipo kwa kuzingatia viwango halisi kama ilivyoainishwa katika miongozo husika.