SERIKALI ipo katika mpango wa kuhakikisha inasambaza magari mawili ya wagonjwa katika kila halmashauri nchini kwa lengo la kuboresha huduma za afya.
Hayo yamesemwa leo Alhamisi na Naibu Waziri wa TAMISEMI, Deogratius Ndejembi bungeni jijini Dodoma katika kipindi cha maswali na majibu.
“Magari haya yanakuja kwa awamu na kila halmashauri tutapeleka magari mawili na gari lingine la tatu kwa ajili ya ‘monitoring and evaluation’ ambalo litakwenda kuhakikisha huduma za afya zinasimamiwa vizuri,” amesema Ndejembi.
Aidha, Ndejembi amesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya afya na ununuzi wa vifaa tiba.
“Ni jitihada kubwa ya mama yetu Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha kwamba tunapata vifaa tiba kuanzia ngazi ya zahanati na vituo vya afya,” amesema Ndejembi.