‘Hamasisheni umuhimu wa kuchukua hatimiliki za ardhi’

NAIBU Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete, amewataka Makamishna wasaidizi wa ardhi nchini kufanya uhamasishaji kwa wananchi, ili wajue umuhimu wa kuchukua hatimiliki za ardhi.
Ridhiwani amesema hayo Desemba 22, 2022 mkoani Dar es Salaam wakati akifungua mkutano baina ya ofisi ya Kamishna Msaidizi wa ardhi mkoa wa Dar es Salaam na kampuni zinazofanya kazi katika miradi ya urasimishaji makazi holela kwa lengo la kutatua changamoto za urasimishaji katika mkoa huo.
“Kama ninyi mtaona kazi yenu inaishia kufanya usajili wa michoro ya mipango miji na kuwawekea mawe wananchi mkaamini mmemaliza kazi hii haitoshi, mnachotakiwa ni kuwa na kazi ya kufanya ya kuhamasisha wananchi kuchukua hati,” alisema Ridhiwani.
Pia ameelezea tofauti kubwa kati ya idadi ya viwanja vilivyowekwa mawe katika mkoa wa Dar es Salaam na vile vilivyotolewa hati na kuielezea hali hiyo kuwa hesabu zake zinakataa kabisa.