Hatima mchungaji mwingine wa ‘mauaji’ kujulikana leo

HATIMA ya Mchungaji Ezekiel Odero inatarajiwa kujulikana leo katika Mahakama ya Shanzu itakapoamua kama atazuiliwa kwa siku 30 akisubiri kukamilika kwa uchunguzi kuhusu vifo katika kanisa lake.

Odero alikamatwa Aprili 27, mwaka huu baada ya kuwapo taarifa za ‘mauaji mengi ya wafuasi wake’ kama ilivyokuwa kwa Mchungaji Paul Mackenzie wa Kanisa la Good News International.

Ofisi ya Kurugenzi ya Mashtaka ya Umma (ODPP) iliwasilisha ombi tofauti la jinai mbele ya Hakimu Mkuu wa Mahakama ya Shanzu, Joe Omido ikitaka mshitakiwa huyo azuiliwe kwa siku 30 ili timu ya uchunguzi ikamilishe uchunguzi na kuwasilisha faili hilo kwa DPP likaguliwe.

Advertisement

Mwendesha Mashtaka, Jami Yamina alisema kuwa kulingana na taarifa za kiintelijensia kuna zaidi ya vifo 100 vilivyotokea katika eneo la Odero kati ya 2022 hadi 2023 na wanaotarajiwa kuwa mashahidi ni wafuasi au waumini wenye nguvu wa mshtakiwa.

Katika hati yake ya kiapo, mpelelezi mkuu, George Muriuki alidai anafanya uchunguzi kuhusiana na uhalifu mkubwa ambao Odero anahusika kwa pamoja na kwa njama inayoshukiwa kutekeleza.

Baadhi ya uhalifu mkubwa unaochunguzwa ni mauaji, kusaidia kujiua, utekaji nyara, itikadi kali, mauaji ya halaiki, uhalifu dhidi ya ubinadamu, ukatili wa watoto, ulaghai na utakatishaji fedha.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *