Hifadhi sita za taifa kutumika mradi soko la kaboni 

JUMLA ya hekari milioni 1.8 katika hifadhi  sita  za taifa zitatumika katika mradi wa soko la Kaboni baada ya Mamlaka ya  Hifadhi za Taifa  (TANAPA) na Carbon Tanzania (CT)  kusaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) unaolenga kutekeleza mradi wa kuleta mabadiliko  hizo ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Makubaliano hayo yamefanyika wakati wa Mkutano wa mabadiliko ya Tabianchi unaoendelea kufanyika Dubai,Falme za Kiarabu ambapo nchi 160 zimehudhuria mkutano huo mkubwa ambapo huo ni mpango mkubwa wa kaboni Ukanda wa Afrika Mashariki.
Hifadhi za Taifa zilizoteuliwa kufanikisha mradi huo ni Burigi iliyopo Wilaya ya Chato, Uwanda wa Katavi, Mto Ugalla, Mkomazi, Mkondo wa Gombe na Milima ya Mahale.
Mkurugenzi Mtendaji, Carbon Tanzania, Marc Baker amesema  mradi huo  utazingatia ulinzi, uhifadhi  na kuimarishwa kwa usimamizi wa maeneo,kulinda mazingira ya asili na rasilimali muhimu za wanyamapori.
“Mradi utaanza na upembuzi yakinifu, ambapo TANAPA na Carbon Tanzania watalenga kubaini kiasi kinachowezekana cha mikopo ya kaboni inayoweza kuzalishwa kutoka kila eneo na kubuni mtindo thabiti wa biashara na mpango wa usimamizi ili kuhakikisha mradi huo unakuwa na uwezo wa kifedha na uendelevu wa muda mrefu ambapo itaweka mfano mzuri wa uwekezaji zaidi katika hifadhi za taifa za ziada kote nchini Tanzania.
Amesema mpango huo utahakikisha uhifadhi wa maliasilia kwani wanauzoefu mkubwa  wa kushirikiana  na ngazi mbalimbali za serikali  kuanzia vijiji hadi wilaya na katika ngazi ya taifa.
“Carbon Tanzania ni kampuni ya kwanza na pekee nchini Tanzania kuendeleza miradi ya kaboni inayozingatia uhifadhi wa misitu na kufanikiwa kufikisha mapato kwa jamii za wenyeji. katika Wilaya za Karatu, Mbulu, Tanganyika, Namtumbo, Tunduru na Kiteto kupitia miradi mitatu ya uendeshaji.”
Amefafanua kuwa Carbon Tanzania itatumia mtandao wake wa uwekezaji wa kimataifa ili kutoa fursa kwa TANAPA kupata mapato ya ziada, kuimarisha uwezo wake wa kusimamia  maeneo ya hifadhi inayoyasimamia.
Marc amesema utiaji saini ni hatua muhimu kuelekea mustakabali wa kijani kibichi na endelevu zaidi kwa mbuga za kitaifa za Tanzania.
“TANAPA na Carbon Tanzania zimejitolea kukuza ushirikiano wenye manufaa ambao sio tu kwamba utalinda urithi wa asili wa nchi lakini pia kuchangia kwa kiasi kikubwa hatua za hali ya hewa duniani,”.
Aidha uwekezaji mwingine wa mradi utatoka kwa kampuni ya Tanzania ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited (MeTL), kampuni ya kilimo, viwanda na biashara iliyoanzishwa miaka ya 1970, yenye uwepo wa kikanda katika nchi 6 kote Afrika Mashariki.
Habari imewezeshwa  na MESHA na Ofisi ya Afrika ya IDRC Mashariki na Kusini.
2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *