Huduma ya Puto sasa kupatikana hospitali binafsi
Dar, Mwanza, Arusha

HUDUMA ya uwekaji puto kwa ajili ya kupunguza unene sasa itapatikana katika hospitali mbali mbali nchini.
Awali huduma hiyo ilikuwa ikipatikana Hospitali ya Mloganzila pekee kwa gharama ya Sh milioni 4.
Hata hivyo, leo Machi 7, 2023, jijini Dar es Salaam, mratibu wa masuala ya upasujia wa urembo au marekebisho mbali mbali katika mwili hapa nchini ‘Plastic Surgery Coordinators Tanzania’ Magreth Mashobe amesema kuwa kwa sasa huduma hiyo itapatika katika hospitali ya Seliani mkoani Arusha, CF hospitali Mwanza na Saifee Hospitali Dar es Salaam.
Amesema lengo ni kusambaza huduma hiyo katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar ili ipatikane sehemu nyingi zaidi ndani ya Tanzania na kuruhusu ushindani wa bei ambao utawapa wateja unafuu wa gharama na vile vile kuweza kuwafikia wengi zaidi.

Kazi kubwa ni kuhakikisha madaktari na hospitali zinakidhi viwango vya kimataifa ikiwemo kupata taarifa sahihi za madaktari tunaowatumia pamoja na takwimu sahihi za hospitali ikiwemo kiwango cha maambukizi na idadi kamili ya vifo.” Amesema na kuongeza
“Niwaombe watanzania kuamini huduma hizi mpya na kuendelea kuzifanyia hapa nyumbani ili kuepuka madhara makubwa ikiwemo kutumia hospitali na madaktari wa nje wasiokuwa na sifa wala mkataba wowote halali na mteja ambapo inapelekea watanzania wengine kuishia kupata madhara makubwa ya kiafya.”Amesema Magreth
Amesema mbali na huduma hiyo ya uwekaji puto pia wanaratibu uduma ya urekebishaji maziwa ama kuyapunguza au kuyaongeza, kupandikiza nywele, huduma ya kurekebisha masikio, pua, na marekebisho mbali mbali ya mwili.
Aidha, Magreth ameishukuru Wizara ya Afya kwa ushirikiano mkubwa ambao wamekuwa wakiwapatia.

“Kwa kipekee kabisa nawashukuru madaktari wetu hapa nchiini kwa mara ya kwanza kabisa Novemba 15 mwaka jana tuliweza kuweka historia ya kuratibu na kupatia vifaa pamoja na kuratibu madaktari wetu kupata ujuzi wa ziada juu ya puto na hivyo kufanikisha hospitali ya Mloganzila kuweza kutoa huduma ya puto.”Amesema
Naye daktari bingwa wa upasuaji kutoka Saifee Hospital Abbas Essajee akizungumza amesema lengo la mtu kuwekewa puto ni kupunguza uzito kilo 15 mpaka 20 kwa miezi sita na inawekwa kwa njia ya ‘Endoscope’ na hakuna upasuaji wowote unaofanyika ni mpira unapitishwa mdomoni ikiwa na puto na camera mbele.
“Puto inapelekwa ndani ya tumbo la chakula na inajazwa maji kwa kiwango fulani, inachukua nafasi ya chakula tumbonii ili mgonjwa akiwa na njaa ya chakula akila anashiba haraka na pia inasaidia chakula kukaa muda mrefu tumboni na hivyo mtu aliyewekewa hatakuwa akisikia njaa na hivyo itamsaidia kuacha kula kula hovyo.”Amesema



