India yaahidi raha wakulima

KAMPUNI na wafanyabiashara kutoka India wataendelea kuwa waagizaji  wakubwa na wanunuzi wa nafaka na mazao mchanganyiko, yakiwemo ya viungo kutoka Tanzania.

Balozi wa  India hapa nchini, Binaya Srikanta Pradhan  amesema hayo  wakati wa majadiliano ya kukubaliana na kuweka ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Taasisi za nchini, India ikiwemo taasisi ya Teknolojia India (ITI).

Amesema Tanzania ni sehemu muhimu ambayo inazalisha mazao ya aina mbalimbali yakiwemo ya korosho, soya , maharagwe mabichi, parachichi na yale ya  viungo ambayo mengi hununuliwa na kampuni kutoka India .

Advertisement

Pradhan amesema ushirikiano  na SUA  utaiwezesha India kufungua milango ya kubadilishana wataalamu kati ya taasisi za vyuo vikuu vya nchini mwake kwenye  sekta ya  uhandisi kilimo, mifugo na uvuvi na uhandisi katika  kilimo cha umwagiliaji.

Amesema kuwa hatua hiyo itawezesha  kuboreshwa uzalishaji katika nyanja hizo na hivyo  kusaidia kuimarisha masoko ya nchini India ,  kukabiliana na changamoto za ubora wa bidhaa zinazozalishwa, ili kupata soko la uhakika nchini humo.

“ Ujio wangu SUA unanipa fursa ya kuangalia vitu gani tunaweza  kuvifanya kwa pamoja ili kuunganisha sekta ya kilimo, tafiti, masoko, mafunzo na teknolojia katika nchi hizi mbili kwa manufaa ya wananchi wa pande zote “ alisema Balozi Pradhan.

Balozi Pradhan amesema faida aliyoipata mara baada ya kutembelea baadhi ya maeneo ya Chuo Kikuu hicho  hususani eneo la  Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Wanyama na Kituo cha Utafiti wa Uchumi wa Buluu,  imeonesha  ya kwamba  SUA imejizatiti katika kuleta maendeleo ya kilimo nchini Tanzania.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Profesa Raphael  Chibunda  ametaja kuwa  mkakati wa maendeleo kwa miaka mitano ijayo ya chuo hicho  kitakuwa cha kuzalisha watu wanaoenda kutengeneza kazi .

Profesa Chibunda amesema  kwa sasa tayari Chuo Kikuu kimekuwa na  Atamizi, kufanya maboresho  ya mitaala pamoja na kuweka mkazo kwa wanafunzi kufanya mafunzo kwa vitendo.

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *