ASKOFU Msaidizi Jimbo la Bukoba, Methodius Kilaini amesema shule za Kemebosi na Kaizirege zimeleta zimeleta ushindani mkubwa na kuwa kielezo cha elimu mkoani Kagera.
Kutokana na hali hiyo, amesema ili shule hizo ziendelee kufanya vizuri, ni lazima walimu waendelee kusisitiza maadili mazuri kwa wanafunzi wao na jamii inayozunguka shule hiyo kwa sababu bila maadili hakuna ufaulu mzuri.
Alitoa kauli hiyo alipokuwa mgeni rasmi katika mahafari ya kidato cha nne na darasa la saba na kusema kuwa, shule nyingi zimepungukiwa na ufaulu baada ya walimu kuvunja maadili na miiko yao ya kazi.
Alisema ameridhishwa na uwekezaji unaofanywa na shule hiyo, ambayo imekuwa ikifanya vizuri katika nafasi za juu kitaifa na kuongeza kuwa miundombinu iliyowekwa shuleni hapo ni mizuri kwa wanafunzi kujifunzia.
Awali Meneja wa shule hizo, Kisha Ilamulila, alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuanzisha ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wanaofanya vizuri zaidi masomo ya sayansi
Alisema fursa hiyo tayari imezaa matunda kwa wanafunzi ambao wamefanya vizuri zaidi kwa kidato cha sita, na wanafunzi 11 wa shule hiyo wamepata ufadhili wa masomo yao, hivyo kuleta chachu kwa wanafunzi waliobaki kufanya vizuri zaidi.
Alisema ufadhili huo, umesaidia kuleta ushindani ambao hauna ubaguzi bali juhudi binafsi ya mwananfunzi mwenyewe, ambapo amewahakikishia wazazi kuwa walimu wanaendelea kufanya vizuri zaidi, ili kuhakikisha watoto wao wananufaika na fursa hiyo.
Alisema shule hiyo kwa kipindi cha miaka 4, ilianzisha ufadhili wa wanafunzi ambao majina yao yanaingia katika nafasi 10 za juu katika mitihani ya kitaifa.

Amesema wanafunzi wanaofanya vizuri kidato cha pili wanafadhiliwa bure na uongozi wa shule miaka miwili, ,wanaofanya vizuri kidato cha nne, wanafadhiliwa mpaka kidato cha sita, lengo likiwa ni shule hiyo kuendelea kufanya vizuri zaidi.
“Wazazi na walezi, niwaambie kuwa shule yetu inafanya vizuri sana, serikali yetu inaendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji katika sekta binafsi.
“Habari njema zaidi kuna watu walikuwa wamejenga fikra kwamba mtoto akisoma shule nzuri hapati mkopo, lakini serikali inawekeza ufadhili wake kwa mwanafunzi anayefanya vizuri zaidi, tuipende serikali yetu na kuiunga mkono, huku tukiwasisitiza watoto wetu kusoma kwa bidii,”alisema Ilamulila.