KAGERA: Kamati ya Bunge ya kudumu ya Biashara Viwanda kilimo na mifugo imebaini kuwepo tatizo la vipimo kwenye maeneo ya mazao ya kilimo kupitia mtindo wa Lumbesa unaomnyonya mkulima.
Kamati hiyo imefanya ziara ya kutembelea Mkoa wa Kagera ikiwa ili kuona shughuli za Wizara ya Viwanda na Biashara lakini pia kuangalia namna Taasisi ya Wakala wa Vipimo katika utendaji wake wa kazi na jinsi wakala wa vipimo unavyosaidia kutoa elimu kwa jamii juu ya kupima bidhaa wanazouza na kununua kwa usahihi .
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Deo Mwanyika amesema Taasisi ya Wakala wa Vipimo ni muhimu kiuchumi na humlinda mlaji na kuhakiki vipimo hivyo wanatambua changamoto ambayo wananchi ,walaji na wazalishaji wanapata katika masuala ya vipimo hasa katika sekta ya kilimo ambapo alimwagiza Naibu Waziri wa Viwanda kuhakikisha wakulima wanaozalisha mazao wanawekewa misingi mizuri ya kuuza mazoa yao kwa njia ya vipimo sahihi.
“Mtindo wa Lumbesa unamnyanyasa mkulima ,mara nyingi wakulima hawapimi mazao yao wao wamekariri vifungashio kwa njia hiyo wanaibiwa sana na hawanufaiki na mazao yao tunaomba Wizara ya Viwanda muliangalie hilo kwa ukaribu na mtafute njia ya kulitatua hatutaki tena mazao yanayonunuliwa kwa Lumbesa “amesema Mwanyika
Ameongeza kuwa sheria iko wazi na wasimamizi wa sheria wapo lakini malalamiko bado hayajaisha licha ya kamati kutoa maelekezo ya kuwataka wakala wa vipimo kuhakikisha utaratibu wa kumlinda mlaji, mzalishaji na mkulima wanalindwa kwa kutokuwa na Lumbesa yaani kuweka ujazo unaozidi kilo100.
Naibu Waziri kutoka Wizara ya Viwanda na biashara, Exaud Kigahe amesema kuwa Taasisi ya Wakala wa Vipimo ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya biashara nchini ikiwa ni pamoja kuhakikisha wananchi wanaendelea kutumia vipimo sahihi na kwa wakati wote.
Afisa mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo, Stella Kahwa amesema kazi yao ni kuhakikisha vipimo vinatumika kwa usahihi pia kuangalia bidhaa mbali mbali zinavyofungashwa kwa viwandani na mashambani hivyo watahakikisha mtumiaji wa mwisho anapata kilicho sahihi.