Kamati yamaliza utata kilo nne za tanzanite

KAMATI ya wataalamu wa ramani mgodini kutoka Chuo cha Madini Dodoma imetoa ripoti kwamba madini kilo nne yalichimbwa mita 650 ndani ya kitalu C kinachomilikiwa na serikali na mwekezaji mzawa, Onesmo Mbise.

Pia kamati hiyo imebaini kuwa mageti yaliyowekwa na kampuni ya Gem & Rock Venture inayochimba katika kitalu B yaliwekwa ndani ya mgodi katika kitalu C.

Ofisa Mfawidhi wa Wizara ya Madini mkoani Manyara, Mernad Msengi amesema kamati hiyo imeagiza kampuni ya Gem & Rock Venture kuwa mageti waliyoweka chini ya ardhi yazingatie leseni husika na madini yaliyozalishwa katika eneo la mgogoro yataendelea kushikiliwa na serikali.

Advertisement

Msengi alisema mgodi huo katika kitalu B utaendelea kusimamisha shughuli za uchimbaji hadi itakaporekebisha makosa yaliyoelekezwa na Wizara ya Madini kuhusu ukiukwaji wa leseni uliofanywa na kampuni ya Gem & Rock Venture.

 

Ofisa Mfawidhi wa Wizara ya Madini mkoani Manyara, Mernad Msengi

Alisema timu hiyo ya wataalamu ilifanya kazi kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama kwenye Wilaya ya Simanjiro, viongozi wa mgodi wa Kitalu C na B na baadhi ya maofisa wa Wizara ya Madini.

Viongozi wa kampuni ya Gem & Rock Venture katika mgodi kitalu B walituhumiwa kuchimba madini katika mgodi kwenye kitalu C kinachomilikiwa na serikali na mwekezaji.

Ilidaiwa kuwa wachimbaji 30 kutoka kampuni ya Gem & Rock Venture katika kitalu B walivamia kitalu C na kutoweka na madini ya tanzanite kilogramu nne lakini maofisa wa Wizara ya Madini Mirerani walifanikiwa kuyakamata na kuyahifadhi katika ofisi ya madini Mirerani.

 

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *