Kampuni  yaiunga mkono Serikali maboresho elimu

KAMPUNI  ya ukandarasi ya Kalpataru  Power Transmission Limited  inayoshughulika na umeme imetoa ufadhili na kujenga jengo la utawala la kisasa  kwa ajili ya matumizi ya ofisi za  walimu wa  shule  ya Msingi  Azimio iliyopo  Manispaa ya Morogoro.

Jengo hilo linagharimu Sh milioni 100. Litasaidia walimu  48  waliokuwa wakikabiliwa na  changamoto ya muda mrefu ya kukaa  katika mavaranda  ya madarasa na nje chini ya  vivuli vya kutokana na uhaba wa majengo kwenye  shule .

Shule hiyo ilianzishwa mwaka 2004 ikiwa ni shule shikizi na baadaye kuwa shule kamili iliyosajiliwa. Jengo hilo la kisasa lina  ofisi ya mwalimu mkuu , mhasibu , chumba maalumu cha kutokea ushauri nasaha kwa wanafunzi pamoja na ofisi mbili za walimu.

Ufadhili huo umechangiwa  kwa asilimia 100 na  meneja wa mradi wa ujenzi wa njia ya umeme wa  Reli ya Mwendokasi (SGR) wa  Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO),  Mhandisi Rosamystica Lutenganya anayesimamia  kipande cha Morogoro- Dodoma.

Mhandisi Lutenganya amesema hayo  wakati wa makabidhiano kwa uongozi wa Manispaa ya kwamba kabla ya kupatikana kwa ufadhili huo na kujengwa kwa jengo hilo  aliguswa kuwaona walimu kikaa  nje na chini ya vivuli vya  miti zikiwa ni  ofisi zao .

“Wakati ninawajibika kusimamia  ujenzi wa line ya umeme ya Morogoro- Dodoma ya matumizi ya reli ya SGR ,kila nikipitia niliwaona walimu wapo nje na kwenye miti zikiwa ni ofisi zao na wengi wao ni wanawake   ,hili lilinigusa na kupata wazo la kuisaidia shule hii ipate jengo la utawala “ anasema Mhandisi Lutenganya

Amesema  Kampuni ya Kalpataru ya nchini India iliyopewa kandarasi ya ujenzi wa njia hiyo inao utaratibu wa kusaidia vitu mbalimbali kwenye jamii .

Alisema baada ya kuona changamoto walizokuwa wakizipata walimu wa shule hiyo aliwasilisha wazo lake kwa  uongozi wa shule hiyo na kwa  idara ya elimu  kwa  kuandika  andiko la kuomba ufadhili kutoka kwa kampuni hiyo ili kujengewa jengo la utawala.

Mhandisi Lutenganya alisema baada ya kuandika andiko na michoro ya  ramani  na makadirio ya fedha kiasi cha Sh milioni 100 na kuwasilisha kwa Menenimeti ya Kampuni ambayo iliridhia  maombi hayo na kutoa fedha hizo zilizotumika kujenga jengo hilo  ulionza  Septemba 2022 na kukamilika Februari 2023.

Makamu wa Rais Kampuni hiyo ,Saroj  Kumar Sahoo  kwa niaba ya menejimenti ya Kampuni hiyo amesema  baada ya kupitia andiko la kuomba ufadhili wa kujengewa jengo hilo , uongozi wa kampuni  uliridhia kutokana na uhalisia wake na kutoa ufadhili wa takribani sh milioni 100.

Sahoo amesema  kupitia jengo hilo amewaomba walimu kulitumia  vizuri na kulitunza  ili  kuwezesha  watoto wapatie elimu nzuri kwa ajili ya maisha yao ya baadae.

Kwa mujibu wa Makamu wa Rais wa Kampuni hiyo ,ufadhili uliotolewa ni kwa mara ya kwanza  tangu imeanza kazi hapa nchini baada ya kukupokea ombi na andiko  hilo.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button