Kasi yazidi Kiswahili kitumike EAC, UN

KASI ya wadau mbalimbali katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuinadi Lugha ya Kiswahili ili itumike katika kanda hiyo, inazidi kuongezeka huku wengine wakisisitiza umuhimu wa kukitumia kutambulisha WanaEAC na kutumika katika Umoja wa Mataifa (UN) ifikapo mwaka 2028.

Wanataka Kiswahili kipewe hadhi inayostahili wakisisitiza Baraza la Mawaziri la Afrika Mashariki kutekeleza haraka maboresho ya Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ili lugha hiyo itumike katika jumuiya hiyo ya kikanda.

Katika maadhimisho ya pili ya Siku ya Kiswahili Duniani yaliyofanyika Julai 7, wadau wametaka EAC kutekeleza mambo yaliyoagizwa na wakuu wa nchi wanachama kuhusu lugha hiyo.

Advertisement

Mbunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) kutoka Tanzania, Dk Abdullah Makame alisema ni vema kukienzi na kukithamini Kiswahili nchini na kwamba ili kulitekeleza hili, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali iandae miswada ya sheria kwa kutumia Lugha ya Kiswahili badala ya kutumia Kiingereza.

“Tunataka kuona Baraza la Mawaziri la Afrika Mashariki likitekeleza maelekezo ya wakuu wa nchi haraka, hususani katika suala la mkakati wa Lugha ya Kiswahili,” alisema Abdullah.

Alitaka serikali zitumie diplomasia na ushawishi kuwezesha Kiswahili kutumika kama lugha rasmi ya Umoja wa Mataifa ifikapo mwaka 2028 na lugha ya kwanza ya Afrika katika umoja huo.

“Hili litasaidia si tu kuikuza lugha yetu, utamaduni wetu na fahari yetu, bali pia kukuza biashara na ajira kwa watumiaji wa lugha ya Kiswahili,” alisema mbunge huyo.

Naye Waziri Mkuu wa Uganda, Robinah Nabbanja alisisitiza matumizi ya Kiswahili katika kutambulisha wananchi wa EAC na umoja wao katika safari ya kuelekea Afrika Mashariki iliyounganishwa.

Kwa mujibu wa Nabbanja, ukanda wa Afrika Mashariki una watu wenye tofauti kubwa ya makabila na lugha akitaja makabila 56 ya Uganda, 42 ya Kenya na zaidi ya makabila 120 ya Tanzania.

Kwa msingi huo, Nabbanja alisema: “Kiswahili kitasaidia kutengeneza utambulisho wa pamoja wa watu wote wa Afrika Mashariki.” Akimwakilisha Rais Yoweri Museveni katika maadhimisho ya pili ya Siku ya Lugha ya Kiswahili Duniani ya EAC mjini Kampala, Nabbanja alisema ili Uganda ishiriki kikamilifu katika EAC, inapaswa kuzingatia jukumu muhimu la Kiswahili katika kukuza ajenda ya ushirikiano wa kikanda kwa maendeleo endelevu.

Katika hafla hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayeshughulikia Sekta za Miundombinu, Uzalishaji, Jamii na Siasa, Andrea Malueth alipongeza juhudi zinazofanywa na Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki (EAKC) kwa kushirikiana na Mtandao wa Vijana wa EAC kuendesha ajenda zao kwa manufaa ya pande zote mbili.

Malueth aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa EAC, Dk Peter Mathuki, alisema inatia moyo Kiswahili katika nchi nyingi za EAC kimepitishwa kuwa lugha rasmi au lugha ya taifa.

“Tunaomba nchi wanachama kuweka juhudi zaidi katika kufundisha Kiswahili katika mfumo wa shule kwani hii itahakikisha vijana wetu wengi wanakua na fikra na mitazamo ifaayo kwa Kiswahili. Pia, tunahimiza vyuo vikuu na vituo vingine maalumu vya ufundishaji na utafiti wa Kiswahili kushirikiana kuimarisha uwezo,” alisema

2 comments

Comments are closed.