MKURUGENZI wa Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS), Yusuph Nassor amechukua fomu ya kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba katika uchaguzi uliopangwa kufanyika Januari 29 mwaka 2023.
Akizungumza baada ya kuchukua fomu leo Desemba 12, Nassor aliyewahi kuwa Mkuu wa Kitengo Cha Fedha, Utawala na Uendeshaji cha Klabu hiyo, amesema ameamua kutumia nafasi yake ya kikatiba, ili kuingoza klabu hiyo kongwe.
“Ninaifahamu vizuri Simba kwani mbali ya kuwa nina mapenzi nayo kwa kipindi kirefu, pia nimefanya nayo kazi vizuri hadi wakati huu nilipoamua kuchukua fomu hii,” amesema Nassor na kuongeza kuwa kwa vile muda wa kampeni bado, wakati utakapofika ataeleza mikakati yake.