KIGOMA; NAIBU Waziri wa uchukuzi, David Kihenzile amezitaka mamlaka na taasisi za serikali zinazotekeleza miradi ya ujenzi wa miundombinu na vyombo vya usafirishaji majini ziwa Tanganyika kutekeleza maagizo na maelekezo ya Rais, Samia Suluhu Hassan ya miradi hiyo kutekelezwa kwa wakati.
Naibu Waziri huyo alisema hayo katika Bandari ya Kigoma alipofanya ziara kutembelea taasisi za usafirishaji za Mkoa wa Kigoma ambapo alikumbushia maagizo ya Raisi Samia aliyotoa alipofanya ziara mkoani humo mwaka jana.
katika ziara yake ndani ya bandari hiyo Naibu Waziri huyo alitembelea na kuona ukarabati wa meli ya mafuta ya MT Sangara sambamba na kupata maelezo ya mpango wa ukarabati wa meli za abiria za Mv.Liemba na Mv.Mwongozo.
Alisema kuwa serikali imetoa kiasi cha Sh trilioni moja kwa aili ya ujenzi na ukarabati wa meli za kubeba abiria, kubeba mizigo,mafuta na uboreshaji wa miundo mbinu ya bandari za ziwa Tanganyika ambapo mipango yote hiyo inalenga kuufanya Mkoa wa Kigoma kuwa na tija kubwa katika kuongeza mapato ya serikali.
Akitoa maelezo kuhusu ukarabati wa meli ya Mt Sangara Meneja wa kampuni ya meli (MSCL), Allan Butembelo alisema kuwa kiasi cha Sh bilioni 8.4 zimetumika kukarabati meli hiyo ambapo ukarabati wake umefikia asilimia 95 na kipindi cha miezi mitano ijayo itakuwa imeanza safari zake katika nchi za Maziwa Makuu.