KILA Novemba 19 huwa ni maadhimisho ya siku ya choo duniani. Katika taarifa ya kuadhimisha siku hii, Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Matshidiso Moeti amesisitiza juhudi ziongezwe zaidi kuhakikisha kila mtu anakuwa na choo salama ifi kapo 2030.
Amesema kulingana na takwimu za Mpango wa Pamoja wa Ufuatiliaji 2020, watu wawili kati ya watatu wanakosa huduma za choo zinazosimamiwa kwa usafi na usalama.
Ripoti hiyo inaonesha kuwa barani Afrika, asilimia 27 ya watu wa vijijini na asilimia tano ya watu wa mijini, bado wanajisaidia pasipo choo.
Wakati takwimu za dunia zikibainisha hayo, hapa nchini taarifa zinaonesha nchi imepiga hatua kutokana na kuwapo ongezeko la vyoo bora huku kaya zisizokuwa na huduma hiyo, zikipungua kwa kiwango kikubwa.
Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Afya, Mazingira kutoka Wizara ya Afya, Anyitike Mwakitalima alitoa taarifa hiyo wakati wa kilele cha wiki ya usafi wa mazingira na mashindano ya usafi mwaka 2022 iliyofanyika jijini Dodoma juzi.
Alisema katika ngazi ya kaya, ongezeko la vyoo bora limetoka asilimia 19.5 mwaka 2012 hadi kufikia asilimia 72.6 mwaka 2022. Kaya zisizokuwa na vyoo zimepungua kutoka asilimia 20.5 hadi kufikia asilimia 1.4 sasa. Tunapoangalia takwimu hizi, zinaleta matumaini kwa maa
na ya kiwango kupungua. Lakini katika uhalisia, hatupaswi kushangilia. Tunaamini kila mdau wa mazingira na afya kwa ujumla, anatamani kutosikia juu ya kuwapo mtu au jamii yoyote iliyoachwa nyuma katika suala zima la matumizi ya choo bora na salama.
Choo duni ni hatari kwa kaya na jamii kwa ujumla kwani kinaweza kusababisha hatari kwa maana ya mlipuko wa magonjwa yatokanayo na uchafu kama vile kipindupindu. Kwa hiyo tunatamani kuona takwimu zinazoonesha kuwa hakuna kaya au jamii yoyote isiyokuwa na choo kilicho salama.
Hata hivyo, tunatambua juhudi ambazo serikali imekuwa ikifanya na inaendelea nazo kufanikisha hili, ikiwamo utoaji elimu na hamasa kwa wananchi kujenga vyoo bora na salama.
Tunasisitiza juhudi hizi ziendelee kwa kasi huku tukihimiza serikali, jamii na wadau mbalimbali kuweka juhudi kuhakikisha suala la choo salama linapewa kipaumbele kama ambavyo pia WHO imeeleza kupitia taarifa ya Dk Moeti.
Tunaunga mkono rai ya WHO kwa nchi mbalimbali ikiwamo Tanzania kuongeza ushirikiano baina ya watunga sera, rasilimali za maji, wataalamu wa usafi wa mazingira na watendaji unapaswa kuongezeka ili suala la umiliki wa choo bora lipate ufanisi.