DAR ES SALAAM : Hospitali ya Agha Khan chini ya ufadhili wa mradi wa kuboresha huduma ya dharura nchini wa ‘Improving emergency care in Tanzania’ (IMECT) kwa kushirikiana na serikali ya Poland imezindua kituo cha mafunzo ya dharura.
Kituo hicho kitatoa huduma kwa watumishi wa afya sambamba na kukabidhi vifaa vya matibabu ya dharura lengo ni kuboresha huduma hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo Balozi wa Poland nchini Tanzania Krzysztol Buzalski amesema anasikia furaha kutoa mchango wa kuboresha sekta ya afya nchini Tanzania kupitia uzinduzi wa kituo hicho huku akiishukukuru ya serikali ya Tanzania kwa ushirikiano inayoonyesha kwa nchi hiyo.
Nae, Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Dk.Gunini Kamba kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa amesema uzinduzi wa kituo hicho cha mafunzo ni msaada mkubwa na utanufaisha watoa huduma ya afya katika ngazi zote na kuahidi kuendelea kushirikiana na hospital ya Aghakan kutoa huduma bora kwa jamii.
Akizungumzia lengo la kuanzisha mradi wa magonjwa ya huduma za dharura Hussein Manji Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura na Mratibu wa Mradi wa IMECT amesema Tanzania haina huduma bora ya dharura na kwamba kituo hicho kitasaidia kuboresha huduma hiyo.
Mmoja wa mnufaika wa mradi huo ambaye ni Mratibu wa huduma ya magonjwa ya Dharura katika hospital Nyamagana Godfrey Kajumbura mbali na kushukuru serikali ya Poland kuwezesha mradi huo amesema katika hospital hiyo takribani watu 69 wamepata mafunzo ya huduma ya dharura kupitia Mradi huo.