Kocha wa Kiduku akusudia kurejesha mieleka

KOCHA wa bondia Twaha Kiduku, Chanz Mbwana maarufu Power Iranda amesema ndoto yake kubwa ni kurudisha mchezo wa mieleka kama atapata msaada kutoka kwa serikali na wadau mbalimbali wa michezo nchini.
Power Iranda amesema ameingia katika ngumi kwa sababu alikosa upinzani katika mchezo wa mieleka lakini kwa sasa anatamani kuurudiasha mchezo huo.
“Kama nitawezeshwa na serikali pamoja na wadau wa sanaa kwa kupata vifaa vya mchezo huo yakiwemo magodoro maalum na vifaa vingine nipo tayari kuurudisha mchezo huo kwa kuanzisha mashindano ya kitaifa hadi kimataifa,” amesema Power Iranda.
Power Iranda amesema pia kama atawezeshwa atawatumia wacheza mieleka wakongwe walioachana na mchezo huo na kujikita katika shughuli nyingine ili kujikimu kimaisha.
“Ninao marafiki zangu wengi tu ambao nilicheza nao miaka hiyo hadi leo wapo nchini na wengine wapo nje ya nchi nao wanatamani kuurusha mchwzo huu lakini hawana uwezo kama mimi,” alisema Power Iranda.
Power Iranda aliitwa jeuri ya Tanzania kutokana na kutokushindwa katika mapambano yake mengi na pia kubeba vitu vizito pamoja na kuvuta magari kwa kutumia meno.