NAIBU Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Ummy Nderianaga amesema kuwa suala la kujiunga na chama chochote cha wafanyakazi ni jambo la hiyari na hakuna mtu yoyote anayelazimishwa kujiunga na vyama hivyo.
Ummy amesema hayo leo Alhamisi 15/6/2023 alipokuwa anajibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu CCM, Rehema Mwandabila lililohoji kauli ya Serikali ni ipi kuhakikisha kwamba kujiunga na uanachama wa vyama vya wafanyakazi ni hiyari, ili kusiwepo kulazimishana kuingia katika vyama hivyo hususani kwa walimu.
“Vyama hivi ni vya kihiyari lakini katiba zao ndio zinawabana pengine ujiunge au ukijiunga utafaidika na kunufaika na kipi, kwa hiyo siyo lazima mtu ajiunge na vyama hivi,” amesema Ummy.
Aidha, Ummy amebainisha kuwa fedha za michango ambazo wanachama wanakatwa mara nyingi huwa zinatumika kusuluhisha migogoro ya kikazi, ikiwemo utetezi katika mahakama za kazi.
Amesema fedha hizo pia hutumika kuongeza bajeti za vyama hivyo, ili viweze kutekeleza majukumu yao ya kikatiba na kisheria kikamilifu kwa wanachama wao.