‘Kuweni na subira ripoti takwimu hali ya ulemavu ‘
OFISI ya Taifa ya Takwimu imewataka wadau wanaohitaji ripoti za takwimu za hali ya ulemavu nchini baada ya matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kuwa na uvumilivu kwani bado taarifa zake zinaandaliwa.
Hayo yamesemwa na Meneja wa Takwimu Mkoa wa Tanga Toni Mwanjota kwa niaba ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Albina Chuwa, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 Kwa viongozi,watendaji na watu wa makundi maalum mkoani Tanga.
Amesema kuwa matokeo ya ripoti hiyo yamekuwa yakisubiriwa kwa hamu kubwa na wadau mbalimbali ,Ili kujua hali halisi ya kundi hilo kwa sasa hapa nchini.
“Taarifa za watu wenye ulemavu ni ripoti ambayo inaandaliwa hivyo tunaomba subira kutoka kwa wadau wote wa takwimu za hali za watu wenye ulemavu,”amesema Mwanjota.
Amesema kuwa ofisi ya takwimu inaelewa umuhimu wa ripoti hiyo ndio maana imo katika orodha ya taarifa ambazo zinaandaliwa kama ambavyo zilizotangulia hapo awali.



