DODOMA: MAMLAKA ua Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), imepewa jukumu la kusajili vikundi vya waendesha bodaboda nchini. Bunge limeelezwa.
Maelezo hayo yametolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa bungeni leo Juni 6, 2024, kwenye maswali ya papo kwa papo, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Aysha-Rose Matembe, aliyetaka kujua mikakati ya serikali kutoa elimu ya usalama barabarani kwa bodaboda ili kupunguza ajali kwa eneo hilo.
Katika majibu yake Waziri Mkuu amesema Serikali imetoa mamlaka kwa LATRA kuanza kusajili maeneo rasmi ya bodaboda kwa nia ya kutoa elimu kuhusu masuala ya usalama barabarani na fursa nyingine mbalimbali zitakazojitokeza.
Pia Waziri Mkuu amesema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia kitengo cha usalama barabarani inaendelea kuratibu utoaji wa elimu ya usalama barabarani kwa waendesha bodaboda, lengo likiwa kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua.