Mabadiliko yaja kuipa mamlaka kamili NEMC

DODOMA: OFISI ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira ipo mbioni kuwasilisha muswada wa mabadiliko ya sheria ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuwa mamlaka kamili, ili kuboresha utendaji wa taasisi hiyo.
Akizunguma leo Aprili 2, 20224 Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Khamis Hamza Khamis amesema hadi kufika Juni mabadiliko hayo ya sheria yatakuwa yameshawasilishwa bungeni.
Amesema mabadiliko hayo yanalenga kutatua changamoto za kiutendaji, kibajeti, kiutumishi na kimuundo zinazolikabili baraza kwa sasa.
Naibu Waziri huyo alikuwa akijibu swali na Maryam Azan Mwinyi, Mbunge Viti Maalum, ambae aliyehoji lini serikali itawasilisha marekebisho ya sheria ya mazingira ili kuipa NEMC uwezo wa hadhi ya mamlaka?
Akijibu Naibu Waziri amesema: “Hivi sasa Ofisi ya Makamu wa Rais ipo katika mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira sura 191, katika marekebisho hayo, kubadili muundo wa Baraza la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na kuwa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA) ni moja ya masuala yanayo pendekezwa kufanyiwa marekebisho, ili NEMC iwe mamlaka,”amesema.