Madaktari 42 Tanzania waimarishwa utoaji huduma

MADAKTARI wa Tanzania 42 wamepatiwa mafunzo ya afya kwa lengo la kuimarisha uwezo wao wa kuwahudumia wagonjwa hususan waishio maeneo ya vijijini.

Kati ya madaktari waliopatiwa mafunzo na Taasisi ya Merck yenye makao yake makuu nchini India, 15 wamewezeshwa njia za kuwasaidia watu wenye changamoto ya kupata watoto huku 29 wakiwezeshwa njia bora ya kukabiliana na magonjwa yasiyo ya kumbukiza.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu Ofiisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo, Dk Rasha Kelej amebainisha kuwa taasisi yake imekuwa ikifanya kazi kwa ukaribu zaidi ya Wizara ya Afya ya Tanzania katika kuwaongezea uwezo wa kazi madaktari na kuwa mbali na hao 42 lakini bado Taasisi hiyo itaendelea kusaidia zaidi sekta ya afya ya nchini.

Advertisement

Amesema,” Merck itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha sekta ya afya na hususan katika kusaidia kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza kama kisukari, moyo, presha na hata masuala ya ugumba ili kuhakikisha nchi inakuwa na watu wasio na changamoto za afya.”

Kwa kuwa magonjwa hayo yasiyoambukizwa ni hatari kwa jamii huku yakiathiri utendaji kazi wao wa kila siku, HabariLeo imezungumza na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima ambaye anabainisha kuwa magonjwa hayo yamekuwa na muingiliano wa moja kwa moja na maisha ya wananchi wa kawaida.

Ametolea mfano wa mwanamke asiyeweza kushika mimba namna ambavyo anaweza kupata changamoto mbalimbali hususan akiwa anaishi kwenye jamii isiyokuwa na elimu ya kutosha kuhusiana na masuala ya afya ya
uzazi anavyoweza kusumbuliwa.

Ameongeza kuwa kwa hatua ya Taasisi ya Merck ya kuwajengea uwezo madaktari juu ya njia bora za kuelimisha jamii namna bora ya kuukabili ugumba itasaidia jamii kuwa imara na kushiriki katika kuwawezesha wasio na watoto kuweza kuwapata.

“Hakika ni msaada mkubwa kuwa na Taasisi kama hii inayowawezesha wataalamu wa afya kusaidia kukabiliana na magonjwa ambayo yamekuwa yakileta athari za moja kwa moja kwa jamii ya watanzania, na ni imani ya wizara kuwa magonjwa hayo yanaenda kukabiliwa” anasema Gwajima.

Taasisi ya Merck kwa sasa inaendelea na kampeni yake ya “More than a Mother” Zaidi ya Mama ambapo Tanzania ni kati ya wanufaika huku nchi nyingine zikiwa ni Angola, Botswana, Burundi, Cabo Verde, Congo, Gambia, Ghana, Liberia, Malawi, Msumbiji, Namibia, Sierra Leone, Zambia na Zimbabwe.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *