AFRIKA lazima iungane kama bara na kuacha kutegemea nchi za nje kwa maendeleo yake, Madaraka Nyerere – mtoto wa Rais wa kwanza wa Tanzania, Julius Nyerere amesema kabla ya kilele cha Mkutano wa wakuu wa nchi na serikali za Afrika na Urusi unaofanyika huko St. Petersberg, Urusi.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anamwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika mkutano huo.
“Nina maoni kwamba kama nchi ina nafasi ya kuongoza kiuchumi, ni mara chache sana itaacha nafasi hiyo kwa hiari,” Madaraka ameliambia Shirika la Habari la Urusi RT, akiongeza kuwa “ni jambo lisilowezekana” kutarajia wengine kujitolea kwa hiari yao katika uchumi wa dunia.
Kwa mujibu wa Madaraka, njia pekee “halisi” ya Bara la Afrika kujiendeleza ni kuungana na kutumia rasilimali zake kwa manufaa ya watu wa Afrika, bila kuwa wakala wa mataifa ya kigeni yanayotaka tu kulinyonya bara hilo kwa manufaa yao.
Pia alisema, kando na kufanya kazi baina ya nchi, mataifa ya Afrika lazima yashirikiane na nchi kama India, Brazil, China na Urusi.
“Vikwazo vinavyowekwa na nchi za Kaskazini katika maendeleo haviwezi kutatuliwa bila ya kuwa na msingi imara wa nchi zinazoanza kuleta msuli wa kiuchumi,” Madaraka alieleza, akisisitiza “hiyo ndiyo njia pekee ya kufuata.”
Katika mahojiano hayo, Madaraka amedai Afrika imekuwa mwathirika wa matakwa ya mashirika ya Magharibi ya kubadili sera zake ili ziendane na zile za IMF na Benki ya Dunia na akapendekeza njia mbadala ambazo jamii zinaweza kufanyia kazi.
Anasema viongozi wa Kiafrika lazima washiriki katika mazungumzo na vijana wa bara hili, ambalo “limezidiwa na maadili na habari kutoka kwa jamii zingine, nje ya Afrika.”
“Tuna hatari ya kupoteza maadili yetu ya kibinadamu na maadili ya haki ambayo tulikuwa nayo hapo awali ikiwa hatutafanya juhudi kubwa kuonyesha kwamba kuna njia mbadala ya jinsi tunavyopanga jamii zetu,” alisema.
Comments are closed.